Maarifa
ya Asili na Haki za Uvumbuzi
Biashara
ya kimataifa katika rasilimali za kijenetiki, ambayo aghalabu hujulikana kama
bio- biashara, siku hizi hufikia madau makubwa ya kiuchumu. Uuzaji wa madawa
ya asili peke yake hufikia zaidi ya Dola za Marekani bilioni 32 (bilioni 1
= milioni 1000) kwa mwaka. Imekadiriwa kwa kuwauliza wenyeji watafutaji madini
(bio – prospectors) wanaweza kuongeza uwiano wa mafanikio kutoka 1 katika
sampuli 10,000 hadi kufikia 1 katika 2. Kwa uzoefu wa mtaalam mwingine, maarifa
ya asili huongeza ufanisi wa kuchuja miti kwa ajili ya dawa kwa zaidi ya asilimia
400. Bila mchango wa maarifa ya asili, madawa mengi muhimu yanayotumika sana
sana yasingekuwepo. Kabla
ya 1992, maarifa na rasilimali za asili vilichukuliwa kuwa ni urithi wa
wanadamu. Hapakuwepo na sheria za kimataifa (na katika nchi nyingi, sheria
za kitaifa) zilizodhibiti ufikio wa rasilimali za kijenetiki. Kutokana
na hali hiyo kulikuwepo na ongezeko la matumizi ya maarifa na rasilimali
za kibiolojia za wenyeji. Kwisha kwa haraka kwa rasilimali za kimazingira
na haja ya kuwazawadia watumiaji na watoaji, kulipelekea uanzishwaji wa
mapatano juu ya Bioanuwai (Convention on Biological Diversity – CBD),
ambayo kwa mara ya kwanza yalitambua thamani ya maarifa na rasilimali
za asili. Mapatano yaliweka utaratibu wa ufikio wa rasilimali za kijenetiki
na wa mgawanyo wa haki na sawa wa faida. Uvumbuzi
ni njia ya kupata umilikaji wa rasilimali fulani mahususi. Kwa kawaida
huhusu ulinzi wa kitu kilichovumbuliwa. Uvumbuzi huo huwa wa vitu vipya
mbalimbali kama vile muziki, riwaya, madawa, programu za kompyuta na matokeo
mengine ya matumizi ya maarifa ya asili. Mapatano
ya Bioanuwai yalianzisha dhana ya haki za uvumbuzi kama mkakati wa kuhifadhi
bioanuwai kwa kuzipatia nchi haki juu ya rasilimali zake. Mpango huu ulijalizwa
na Mkataba juu ya Haki za Uvumbuzi za Kibiashara (Agreement on Trade –
Related Intellectual Property Rights – TRIPS). Kujumuishwa kwa Mkataba
wa “TRIPS” katika mfumo wa WTO kulianzisha masomo mapya kwa nchi nyingi
kuhusu hataza, hatimiliki, alama za kijiografia, majina ya kibiashara
na ubunifu wa viwanda. Lengo kuu la Mkataba ni kuweka kiwango cha kimataifa
cha ulinzi wa haki za uvumbuzi. Haki
za Uvumbuzi:mgogoro au nguvu zaidi
Je,
ulinzi wa maarifa na rasilimali za asili kupitia haki za uvumbuzi huongeza
ama huzuia upelekaji sawa wa faida za kiuchumi kwa wavumbuzi? Wahakiki
wanadai kwamba haki za uvumbuzi ni tishio kwa bioanuwai kwa vile huzuia
ufikio wa rasilimali na wa mazao yanayotokana na rasilimali hizo. Haki
hizo huyafanya makampuni kuwekea hataza uvumbuzi unaotokana na maarifa
na rasilimali za asili, bila kugawana kwa usawa faida za kibiashara na
jumuiya zinazohusika na uvumbuzi. Watetezi wa Mkataba wa “TRIPS” hudai
kwamba mkataba huo kuhamasisha uhumishaji wa teknlojia, ambao unaweza
kuwa mkakati mmojawapo wa ugawanaji sawa wa faida. Yapo masuala mengine
kadhaa ambayo huibuka katika mjadala huu. Haya yatazingatiwa na kurekebishwa
kwa kuangalia mikakati ya kufanya kazi kwa kutumia haki za uvumbuzi zilizopo
na, pale inapowezekana, kuzipanua zaidi kwa lengo la kuhifadhi maarifa
ya asili na bioanuwai. Matatizo
ya utumiaji Hali
ya ubinafsi wa haki za uvumbuzi huleta matatizo kadhaa zinapotumika kwa
jumuiya. Haki hizi hushindwa kuzingatia ukweli kwamba jumuiya huwa na
mkabala jumlifu kwa mazingira yake. Jumuiya za namna hii huona vigumu
sana kuzichukulia rasilimali wanazozitegemea kwa maisha yao kuwa rasilimali
mahususi za kiuchumi na kijamii. Mintarafu
haki za uvumbuzi, jambo hili hupelekea kwenye tatizo jingine kubwa. Jinsi
gani mtu afasili uvumbuzi na wafaidikaji wa uvumbuzi huo katika jumuiya,
ikizingatiwa haja ya kuthibitisha upya na udhahiri wa hicho kilichovumbuliwa.
Katika jumuiya nyingi za kimapokeo, watu hujifunza maarifa kwa muda mrefu
na kuyasambaza kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Kwa njia hiyo, haya
maarifa daima hukua na kubadilika. Hivyo ni vigumu kubaini ni lini hasa
maarifa fulani yaligunduliwa na lini yaliingia kwenye jumuiya. Sehemu
ya pili ya tatizo hili inahusisha ujumuiya wa maarifa ya asili. Ukuzi
wa maarifa huchangiwa na wanajumuiya kama vile wazee ambao hekima na uzoefu
huongeza thamani ya maarifa hayo. Kwa hali hii maarifa daima yamechukuliwa
kuwa ni ya jumuiya na hivyo kushindwa kupata kigezo cha udhahiri wa hataza.
Na endapo jumuiya nzima inahusika na ukuzi wa maarifa ya kimapokeo, mvumbuzi
binafsi atatambulika vipi? Tatizo huwa kubwa zaidi pale ambapo maarifa
ya asili yaleyale hutumiwa na jumuiya mbalimbali duniani kote. Kwa mfano,
kama mitishamba fulani hutumiwa na Wamasai nchini Kenya, na pia Wahindi
wa Amazoni, mvumbuzi halisi wa mitishamba hiyo atatambulika kwa kutumia
njia ipi? Matatizo
yaliyojadiliwa hapo juu yanaweza kupatiwa ufumbuzi kupitia mkataba wa
“TRIPS” kwa kutumia namna mbalimbali za haki za uvumbuzi. Hizi hujumuisha
alama za kijiografia ambazo hutumiwa zaidi kwa uvumbuzi unaofanywa na
jumuiya. Njia nyingine ni kupanua dhana ya haki za uvumbuzi ili kujumuisha
haki zenye msingi wa kijumuiya. Hii yaweza kujumuisha aina za kipekee
za ulinzi zenye ubunifu zaidi kuliko matumizi ya hataza. Zaidi
ya hapo, uanzishaji wa rejista za maarifa ya kimapokeo za kitaifa, kikanda
na kimataifa utawezesha ugawanaji mzuri wa faida miongoni mwa viwanda
na jumuiya. Rejesta hizo zitasaidia juhudi zinazohusu haki za uvumbuzi
kama vile kuimarisha hadhi ya maarifa ya kimapokeo kama sanaa awali, na
hivyo kuwezesha kuwepo kwa “machapisho yanayolindika”. Licha
ya hataza, zipo njia nyingine za kuanzisha haki za uvumbuzi kwa maarifa
na rasilimali za asili. Hizi zinajumuisha alama za kijiografia (majina
ya mahali au maneno yanayohusiana na mahali yanayowezesha kutambua asili,
aina na ubora wa kitu kilichovumbuliwa kwa mfano “chai ya Darjeelina”).
Alama hizi ni nzuri kutunzia mapokeo ya pamoja huku zikiruhusu kutokea
mabadiliko. Zinasisitiza mahusiano kati ya tamaduni za kibinadamu na mazingira
yao na huweza kuhifadhi kadiri mapokeo ya kijumla yatakavyodumu. Haijali
kama mvumbuzi ni mtu binafsi, familia ama shirika kubwa. Jumuiya za wenyeji
hudai maarifa yao yasichukuliwe hivihivi tu kiholela. Hali kadhalika,
alama ya kijiografia hufanya uvumbuzi usihamishwe kiholela. Aina
nyingine za ulinzi ni pamoja na hatimiliki na siri za kibiashara. Hatimiliki
aghalabu hutumika kuzuia sanaajadiia ya kimapokeo isinakiliwe bila ruhusa
maalum. WIPO imelinda sanaajadiia kutoka sehemu mbalimbali za dunia kama
hatimiliki. Siri za kibiashara ni mbinu ya kulinda taarifa za siri zinazoweza
kuwapatia wengine, kama vile mashirika ya kibiashara, unafuu wa ushindani.
Siri hizi zinaweza kuwa njia thabiti ya kulinda maarifa ya asili. Jumuiya
enyeji zingedhibiti ufikio wa maeneo na taarifa kwa watu wa nje kwa kutumia
mikataba inayohakikisha kuwepo kwa siri na faida za kiuchumi. Mbinu za
aina hii zimeshaanzishwa katika nchi kama vile Ecuador kwa msaada wa Benki
ya Maendeleo ya Amerika (Inter – American Development Bank). Jambo
la pekee:ufikio na ugawaji sawa wa faida Baadhi
ya mabishano makubwa yanayohusu haki za uvumbuzi ni yale ya ulinzi wa spishi
za mimea. Mkataba wa “TRIPS” unasema kwamba nchi wanachama zinaweza kutoingiza
kwenye hataza “mimea na wanyama isipokuwa vidubini (vijiumbe) na hasa mifanyikotendani
ya kibiolojia kwa ajili ya uzalishaji wa mimea na wanyama isipokuwa ile isiyo
ya kibiolojia na ya kimikrobiolojia. Hata hivyo, nchi wanachama zitalinda
mimea mbalimbali ama kwa kutumia hataza au mfumo thabiti wa kipekee au mbinu
zozote mchanganiko”. – (Kifungu 27.36). ‘Mfumo
wa kipekee’ ni mbinu za ulinzi ambazo hazitumii hataza. Mbinu inayojulikana
sana ni ile inayohusisha “haki za wazalishaji wa miti”. Katika kiwango cha kimataifa, nchi kadhaa zimejiunga
katika Umoja wa Kimataifa wa Ulinzi wa Aina Mpya za Mimea (International
Union for the Protection of New Varieties of Plants – UPOV) na baada ya
majadiliano zikafikia makubaliano ya Ulinzi wa Aina Mpya za Mimea (Convention
for the Protection of New Varieties of Plants). Makubaliano haya yameweka
viwango vya chini kabisa vya ulinzi ambavyo vyapaswa kuzingatiwa na kila
nchi. Pia huwawezesha wazalishaji miti kufaidika na “marupurupu ya wazalishaji”
ambayo huwapa uhuru wa kutumia mimea inayolindwa katika programu zao za
uzalishaji miti ili kuzalisha aina mpya za mimea. Aina
hii ya ulinzi inaelekea kupingwa na baadhi ya nchi zinazoendelea, lakini
bila sababu za msingi. Kwa mfano, hofu kwamba wakulima hawataruhusiwa
kuendelea na kilimo chao cha kimapokeo kutokana na njia hizi za ulinzi
wa mimea, haina msingi wowote. Zao au jambo ambalo limekuwa likitumika
wazi na umma sio jipya na hivyo haliwezi kupatiwa hataza. Ni aina mpya
tu za mimea ndizo zitakazolindwa, na hata hivyo ni jukumu la mzalishaji
miti kutafuta ulinzi huo. Ulinzi si jambo la lazima. Hivyo, wakulima wataweza
kuhifadhi mbegu kutokana na mavuno yao kwa ajili ya kupanda kwenye ardhi
yao (hii hujulikana kama “marupurupu ya wakulima”). Watu
wengine wanadai kuwa mfumo wa “ulinzi wa kipekee” ambao unaruhusu kuwepo
kwa ubunifu zaidi katika ulinzi wa mavumbuzi, unapaswa upanuliwe zaidi
ili ujumuishe haki za kijumuiya na haki za rasilimali za kimapokeo. Mashirika
yasiyo ya kiserikali kama vile Mtandao wa Dunia ya Tatu (Third World Network)
yanatetea haki mbadala zinazoakisi utamaduni na maadili ya jumuiya enyeji.
Mashirika haya yanadai kwamba ili kuzingatia ipasavyo nguvu ya mabadiliko
ya maarifa ya kimapokeo, dhana ya “ubunifu” yapaswa kufasiliwa kwa mapana
zaidi ya dhana ya ubunifu wa viwandani. Ufasili huo waweza kuzingatiwa
kwenye haki za kijumuiya. Wataalamu
wametoa mkabala jumulifu zaidi unaounganisha haki za uvumbuzi na sheria
na mazoea ya kijadi. Wanadai kuwa maarifa ya asili hayawezi kutengwa na
haki nyingine za asili kama vile haki za binadamu, haki za kumiliki ardhi
na kuwa na serikali huru. Suluhisho mojawapo lingekuwa kuwa na mkabala
unganishi kwa kuanzisha haki za rasilimali ya kimapokeo ambazo zingezingatia
kwa dhati misingi ya haki za jumuiya. Haki hizi zinaweza kuwa mwongozo
wa kuanzisha haki nyingine kama vile haki za uvumbuzi wenye nguvu zaidi. Haki
za uvumbuzi zinaweza kuwa njia inayofaa ya kulinda mifumo ya maarifa ya asili
na mimea ya aina mbalimbali. Hali hii huhimiza umuhimu wa kuyaweka maarifa
ya asili katika maandishi; ambayo baadaye yanaweza kutumiwa kupinga dai la
kutoa hataza kwa maarifa ambayo tayari yanajulikana katika jumuiya. Pili,
inasisitiza umuhimu wa aina nyingine za haki za uvumbuzi licha ya hataza kama
vile alama za kijiografia. Hizi zaweza kuhitajika zaidi na jumuiya za kimapokeo
zinazohitajika kudhibiti ufikio wa rasilimali zake, kwani zinaweza kutumika
kwa maarifa yanayoendelea kubadilika kutokana na mchango wa jumuiya enyeji.
Hii inatupelekea kwenye uwezekano wa kupanua Mkataba wa “TRIPS” ili kuhakikisha
kwamba hataza zinaonyesha chanzo cha rasilimali za kijenetiki na cha matumizi
ya maarifa ya asili na zinazingatia “njia za kipekee” za ulinzi wa haki za
uvumbuzi kama zile za kijumuiya ili kuwezesha upatikanaji wa mgawano sawa
wa faida. *Makala hii iliandikwa na Siddharta Prakash, Mshauri wa Kanda ya Afrika ya Benki ya Dunia. Imechapishwa tena, ikiwa imefupishwa, kwa ruhusa ya mchapishaji wa awali: “Towards a synergy between biodiversity and intellectual property rights”, na S. Prakash, Septemba 1999, Journal of World Intellectual Property (Jarida la Haki za Uvumbuzi), Vol. 2, No. 5 |