THE WORLD BANK GROUP A World Free of Poverty
Home

[Back to TOC]

Ghana: Huduma za Mikopo kwa Wafanyabiashara katika Sekta Isiyo Rasmi

Mtandao wa Action Reseach wa taasisi za kukopesha mitaji midogo nchini Ghana huyakutanisha pamoja mashirika ambayo yanajihusisha na utoaji mitaji/mikopo ya mitaji kwa wananchi maskini wa Ghana. Kwa msaada wa Benki ya Dunia, mtandao huu ulifanya utafiti ambao, ulitoa maelezo mafupi juu ya ubunifu usio rasmi, ulio rasmi kidogo na rasmi kabisa (uliofanywa na taasisi za kukopesha mitaji midogo) ambao umeanzishwa katika utoaji wa mikopo kwa wafanyabiashara wanawake wa Ghana. Utafiti huo pia unatoa mapendekezo ya kuboresha na kuimarisha utoaji wa huduma hiyo.

Utaratibu wa Utoaji wa Huduma za Mikopo inayowalenga Wanawake

Kwa sababu za kijamii na kiutamaduni na sababu nyinginezo, wanawake, walipokuwa wasichana walinyimwa fursa ya kupata elimu na hata wale waliofanikiwa kupata elimu, walipata elimu ya ngazi za chini. Ukosefu huu wa elimu umezuia uwezo wao wa:

·         Kupata ujuzi na utaalamu wa kuweza kujiajiri.

·         Kuwa na fursa ya kupata taarifa juu ya huduma za kimisaada za kuboresha biashara zao.

·         Kupata mapato na hivyo kuweza kukuza mitaji yao.

Kwa ajili ya vikwazo hivi, wanawake wengi wa vijijini wamekuwa wakijihusisha na shughuli za ulimaji wa mazao ya chakula na shughuli zinazowapatia kipato kidogo; wakati wanawake maskini waishio mijini wanaendesha biashara ndogo ndogo katika sekta isiyo rasmi. Shughuli hizi zimesaidia kidogo na wakati mwingine hazijasaidia kabisa. Hii ni kwa sababu shughuli zenyewe za kibiashara zinakua kidogo au hazikui kabisa na hivyo kufanya wanawake wengi kuwa kwenye kundi la maskini na wengi wao kupatiwa mikopo na taasisi za kukopesha mitaji midogo. Baadhi ya taasisi hizi zinalenga kuwahudumia wanawake kwa sababu imethibitika kuwa njia hii ni ya moja kwa moja ya kupunguza umaskini na kuongeza ustawi wa familia kwa ujumla.

Katika programu za taasisi za ukopeshaji mitaji midogo ambazo zinalenga wanawake na wanaume, mitaji inayotolewa kwenye biashara zinazoendeshwa na wanawake ni midogo ukilinganishwa na ile inayotolewa kwa wanaume. Katika maeneo ya vijijini, taasisi chache za fedha zinawakopesha wanawake wafanyabiashara. Isipokuwa pale taasisi inapokuwa na sera mahususi ya kutenga fungu kubwa la mkopo kwa wanawake, kiasi cha mikopo kinachotolewa kwa wanaume bado kitaendelea kuwa kikubwa ikilinganishwa na kile kinachotolewa  kwa wanawake. Lakini na hata hivyo, mara nyingi wanawake wamekuwa warudishaji wazuri wa mikopo kwa kiwango kikubwa kuliko wanaume.

Wakopeshaji wa mikopo kwa wanawake aghalabu ni vikundi visivyo rasmi kama vile wakusanyaji wa fedha wa kikundi cha Susu na ROSCAS; na wakopeshaji wasio rasmi sana kama vile mashirika yasiyo ya kiserikali na vikundi vya kijamii (CBOs). Wakopeshaji rasmi ni Benki za Akiba na Mikopo, Benki za Vijijini na Jamuiya na vyama vya ukopeshaji. Pamoja na taasisi hizi , programu za sekta ya umma zimeanzisha huduma za mikopo na zinginezo kwa ajili ya walengwa.

Huduma za mikopo na huduma nyinginezo

Uhamasishaji wa uwekaji wa akiba na utoaji wa mikopo ndio huduma za kimsingi zinazotakiwa kufanywa na taasisi hizi mbalimbali. Riba inayopatikana kwenye akaunti za akiba ni asilimia 25 – 35 kwa mwaka. Kiwango cha riba za mikopo kinaanzia asilimia 20 (kwa mikopo yenye ruzuku) na kufikia asilimia 50 (kiwango cha kibiashara).

Huduma zisizo za kifedha kama vile uto

aji mafunzo ya uendelezaji na ukuzaji wa biashara, ukuzaji wa ujuzi na stadi za kibiashara na huduma za ustawi wa jamii kama vile uzazi wa mpango hutolewa na baadhi ya taasisi za kukopesha mitaji midogo midogo. Taasisi hizi zina lengo la kujenga uwezo wa wafanyabiashara wadogo wadogo na kuwaendeleza kwa kuboresha utumiaji na ulipaji wa mikopo na ustawi wa maskini kwa ujumla.

Mafanikio ya Programu zilizopo

Ili kuhakikisha hali ya uendelevu na kukidhi mahitaji ya wateja, taasisi za kukopesha mitaji midogo midogo zinatumia njia mbalimbali katika utoaji wa huduma hizo. Njia hizo ni pamoja na njia ya kutumia vikundi, ushawishi kwa kutumia vikundi vya marika, utoaji wa mikopo na uwekaji wa akiba, kama fedha taslimu za ziada. Mbinu hizi zimesaidia kuhakikisha ulipaji wa mikopo unaongezeka kwa kiwango kikubwa.

Udhaifu wa programu zilizopo

Taasisi nyingi  za ukopeshaji mitaji zinapata matatizo ya kiutendaji ambayo yanaathiri uwezo wa taasisi hizo kukuza huduma zake za kifedha. Matatizo hayo ni pamoja na kuwa na msingi wa mtaji ulio dhaifu; mfumo mbaya wa usimamizi wa mikopo inayotolewa kutoka kwenye fedha zilizowekwa kwenye akaunti za akiba; kuwepo mfumo dhaifu wa  usimamizi wa taarifa; kuwepo kwa fungu la mkopo lisilotosheleza mahitaji ya walengwa; na ukosefu wa nguvukazi na fedha za kusaidia kufanya ufuatiliaji wa mikopo.

Mbinu za vijijini na zile za mjini

Taasisi za fedha zinazotoa mitaji midogo midogo zinazolenga wanawake wa vijijini, zinatumia mbinu za kukopesha wanawake waliopo katika vikundi ili kuhakikisha uwajibika wa pamoja katika kutumia vizuri mikopo. Mbinu hii imeonekana kuwa ya manufaa na hivyo kuongeza idadi ya wateja wanaohudumiwa na mpango huu. Hii imeonekana ni muhimu katika kupunguza gharama ya kufikia jamii za vijijini zilizojitenga. Mafunzo ya uundaji vikundi pia yanawapa wanawake wa vijijini ujuzi wa uongozi na wa  kufanya maamuzi. Wanachagua wajumbe wa kuunda vikundi, wanafanya maamuzi yahusuyo mikopo na vilevile wanashiriki katika uendeshaji wa ndani wa taasisi zinazotoa mitaji midogo.

Mbinu zinazotumika mijini

Taasisi za kukopesha mitaji midogo zilizopo mijini zinalenga katika utoaji mikopo kwa mtu mmoja mmoja kwa vile jamiia za mjini haziishi kwa ukaribu sana kama zile za vijijini. Wateja wa taasisi hizi za mijini kwa kawaida huenda wao wenyewe kwenye taasisi husika kwa huduma za mikopo. Lakini katika maeneo ya vijijini taasisi hizi huwa zinawafuata wanavijiji walipo na hivyo kufanya taasisi za mijini kuwa na gharama ndogo za uendeshaji wa shughuli za kibenki.

Taasisi za kukopesha mitaji za Kaskazini na Kusini mwa Ghana

Aina zote za taasisi za utoaji mikopo, yaani  zisizo rasmi, zilizo rasmi kidogo, zilizo rasmi kabisa na programu za sekta ya umma zinapatikana Kaskazini na Kusini mwa Ghana. Taasisi za watu binafsi, kama vile benki za akaunti za akiba na za kutoa mikopo zhupatikana zaidi Kusini mwa Ghana. Hii inatokana na kuwepo kwa idadi kubwa ya watu na shughuli za kiuchumi ambazo zinawahakikishia wenye mabenki uendeshaji wa mabenki kwa gharama ndogo. Kaskazini mwa Ghana kuna programu nyingi za sekta ya umma zinazopata ruzuku kutoka serikalini.

Ubunifu uliofanyika

Mahusiano ya Wakusanya fedha wa Susu na mabenki katika utoaji mikopo

Wakusanyaji fedha wa kikundi cha Susu wanaendesha shughuli zao katika maeneo ya vijijini na mijini ya Ghana kama mawakala wanaojitegemea. Kwa desturi, waendeshaji wa Susu huwa ni  wanaume. Lakini hata hivyo, wanawake wachache wamejiunga na taalamu hii, ingawaje hakuna taarifa yoyote kuhusiana na idadi yao au uwiano wao na wanaume. Chama cha Ushirika cha Wakusanyaji wa Susu, kijulikanacho kama GCSCA, kilichoanzishwa mwaka 1990,  kimekuwa kikijaribu kuhamasisha, kuratibu na kudhibiti shughuli za uendeshaji wa Wakusanyaji wa Susu ambao wakati mwingine shughuli zao zimeonekana kuwa za udanganyifu. GCSCA imebainisha malengo ya Wakusanyi hao kama ifuatavyo:

·         Kutoa huduma ya ukusanyaji wa fedha za akaunti ya akiba kutoka kwa mtu mmoja mmoja na kwenye vikundi vya maeneo ya vijijini na mijini.

·         Kutoa huduma sahihi za kibenki kwa kuwaunganisha wafanyabiashara wadogo wadogo na sekta zisizo rasmi, ambao hawawezi kuacha shughuli zao za kibiashara na kufanya safari ili kuweza kukutana na wafanyabiashara wengine waliopo katika sekta isiyo rasmi.

·         Kuwajengea tabia ya uwekaji akiba maskini wa vijijini na mijini.

·         Kutoa nafasi ya kuiunganisha sekta rasmi inayoojihusisha na shughuli za kibenki na wafanyabiashara wadogo; na

·         Kutoa nafasi kwa watu kuweza kujiajiri wenyewe kama wakusanyaji wa fedha wa Susu.

Uhamasishaji wa Uwekaji akiba

Utaratibu wa kawaida wa kuhamasisha uwekaji wa akiba kutoka kwa wateja ni ule wa watumishi wa kikundi cha Susu kukusanya malipo kidogo kidogo yanayotakiwa kukusanywa kwa mpangilio wa kila siku ama kila juma. Mwishoni mwa mzunguko, yaani baada ya siku thelathini (30), kiasi cha fedha kilichokusanywa kinalipwa kwa mteja ukitoa kiwango kinachokusanywa kwa siku moja ambacho hubakia kwa wakusanyaji wa Susu kama malipo au faida yao. Katika jaribio la kutoa huduma inayowalenga wateja, karibu wakusanyaji wote wa Susu wameanza kuhamasisha ukusanyaji wa fedha kuanzia mchana kila siku. Ukusanyaji wa aina hii unawapa wateja nafasi ya kufanya biashara na kupata kiasi cha fedha kabla ya kuweka akiba. Mbinu hii imeonekana kuwa muafaka kwa wanawake maskini wa mijini na vijini ambao kipato chao ni kidogo sana kuweza kuweka kiasi kikubwa cha fedha kwenye taasisi za fedha zilizo rasmi.

Masoko ndio maeneo yenye shughuli za biashara hasa zile zinazoendeshwa na wanawake. Masoko haya yanatoa nafasi nzuri ya wakusanyaji wa Susu kufanya kutoa huduma zao kwa gharama ndogo. Kiasi cha fedha kinachopatikana kwa siku kinawekwa kwenye sefu majumbani au huwekwa kwenye benki za biashara zilizo karibu kwa mtindo ule ule wa kuweka kila siku.

Wakusanyaji wa Susu wakati mwingine huwa wanawakopesha wateja wao  wenye tabia ya kuweka pesa kila siku ili waweze kulipa ada za shule, gharama za matibabu n.k.

Mipango inayofanywa kwa kushirikiana na asasi za fedha

Baadhi ya taasisi za fedha na mashirika yasiyo ya kiserikali hivi sasa wanafanya mipango ya kushirikiana na wakusanyaji wa fedha wa kikundi cha Susu. Taasisi hizi ni pamoja na Benki ya Vijijini ya Nsoatreman, Benki ya Maendeleo ya Kilimo, Benki ya Akiba na Mikopo ya Citi, na Action Aid ya Ghana.

BENKI YA VIJIJINI YA NSOATREMAN (NRB). Katika mpango wa majaribio uliofanywa na Benki hii, Benki iliwakopesha kwa masharti nafuu  baadhi ya wakusanyaji wa fedha wa Susu ambapo nao baadaye waliwakopesha wateja wao na kupata malipo ya kazi hii kutoka Benki hii. Benki ya Vijijini ya Nsoatreman imekubaliana na wakusanyi hao juu ya kiwango cha malipo wanayopata kutokana na riba inayopatikana kutoka kwenye fedha zinazowekwa kwenye akaunti za akiba. Katika jaribio la awali lililofanyika mwaka 1997, Benki ilitenga kiasi cha dola za kimarekani 732 kwa kila mkusanyi wa Susu aliyechaguliwa.

BENKI YA MAENDELEO YA KILIMO (ADB). Benki ya Maendeleo ya Kilimo kwa kutumia tawi lake la Sunyani la Mkoa wa Brong Ahafo imeanzisha mpango wa utoaji wa huduma za kifedha kwa kushirikiana na Tata Susu Maalum. Fedha zinazopatikana baada ya uhamasishaji uliofanywa na Tata Susu Maalum hupelekwa benki ambako kitengo maalum kimetengwa kuwahudumia wakusanyaji wakati wa muda wa kawaida shughuli za kibenki. Kwa sasa hivi kuna mpango wa kupanua utaratibu huu kwa miji mingi zaidi ya vijiji vilivyopo karibu na Sunyani.

BENKI YA AKIBA NA MIKOPO YA CITI. Benki hii imeanzisha mradi wa majaribio wa utoaji wa mikopo kwa kushirikiana na Tawi la Greater Accra la GCSCA. Katika mradi huu, wakusanyaji fedha wa Susu wenye akaunti kwenye tawi lolote la Benki ya Akiba na Mikopo ya Citi wanaweza kupewa mikopo ya muda mfupi. Mikopo hii hutolewa kwa lengo la kuwawezesha wakusanyaji watoe malipo ya awali kwa wateja wao kama watayahitaji.

ACTION AID GHANA. Utaratibu ulioanzishwa na Action Aid Ghana kwa kushirikiana na Wakusanyi wa Susu huko Kaskazini ya Ghana umetoa fursa ya kuinganisha sekta ya huduma za kifedha isiyo rasmi na jamii za vijijini. Katika utaratibu huu jamii zinazoshiriki katika programu ya mkopo ya Action Aid za Bawku, Cheriponi na Tamale zinachagua wakusanyaji kutoka katika kikundi cha Susu. Wakusanyaji hawa hutoa huduma za kukusanya akiba na mikopo majumbani kwa wateja na mikopo iliyolipwa hupelekwa kwenye Action Aid.

MASHIRIKA YASIYO YA KISERIKALI

UHURU KUTOKA KWENYE NJAA (FREEDOM FROM HUNGER – FFH). Freedom From Hunger ni shirika lisilo la kiserikali la kimataifa ambalo linashirikiana na taasisi sita za Ghana za kukopesha mitaji midogo midogo ambazo zina programu za kutoa mikopo yenye lengo la kupunguza umaskini na inayowalenga wanawake. Vigezo vinavyotumika kuchagua taasisi za kukopesha mitaji midogo midogo za kushirikiana na shirika hili ni:

·         Taasisi lazima iwe na uwezo mkubwa wa kiuongozi na  usimamizi unaohitajika katika kuendesha programu.

·         Taasisi lazima iwe na utaratibu mzuri wa kufikisha huduma zake kwa wanawake walengwa.

·         Taasisi lazima ikubali kutoa watumishi wake kwa ajili ya mafunzo ya uendeshaji wa mikopo yanayotolewa na Shirika la Freedom From Hunger.

 

Taasisi sita zinazofanya kazi kwa kushirikiana na Freedom From Hunger ni

Benki ya Vijijini ya Lower Pra – iliyopo Mkoa wa Magharibi

Benki ya Vijijini ya Brakwa – iliyopo Mkoa wa Kati

Benki ya Vijijini ya Nsoatreman – iliyopo Mkoa wa Brong Ahafo.

Benki ya Wanawake ya Dunia/Ghana – iliyopo mkoa wa Greater Accra

Benki ya Jamii ya Builsa – iliyoko mkoa wa Mashariki ya Juu.

Malengo ya Programu

Malengo ya programu ya Freedom From Hunger ni

·         Kutoa mikopo kuwepo kwa wanawake walio maskini.

·         Kutoa elimu ya afya na lishe.

·         Kutoa elimu ya uzazi wa mpango na kutoa taarifa.

·         Kujenga uwezo wa taasisi za kizawa zinazotoa mitaji midogo midogo kwa kuzingatia mafunzo na msaada wa kiufundi.

Wateja Walengwa. Programu za Freedom From Hunger zinatekelezwa kwa kushirikiana na taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo zinazowalenga wanawake tu kwa sababu zifuatazo: (i) matukio ya umaskini yameonekana zaidi kwa wanawake, (ii) kuongezeka kwa kipato cha wanawake kubadilisha hali ya maisha ya familia, na (iii) shughuli zinazoingiza kipato zikifanywa na wanawake huhitaji mtaji mdogo.

Mbinu za kiutendaji:Freedom From Hunger inatoa mafunzo kwa waendeshaji wa mikopo walioteuliwa kutoka kwenye taasisi zinazotoa mikopo midogo midogo katika nyanja za uanzishaji wa biashara ndogo ndogo; kutoa elimu ya afya na lishe, uzazi wa mipango; usimamizi wa fedha; upagaji wa bajeti na uandaaji wa mipango.

Taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo kwa upande mwingine zina jukumu la kuanzisha  vikundi vya wanawake na kuvipatia mafunzo na huduma nyingine zinazohitaji msaada. Wanachama wa kikundi hulazimika kuweka akiba (kima cha chini hupangwa na wanakikundi wenyewe) kwa muda usiopungua majuma sita. Mikopo hutolewa kwa wanawake kwa riba ya kibiashara ya kati ya asilimia 48 na 51. Amana zao za akiba hutumika kama fedha taslimu za ziada. Mkopo huchukua majuma 16 na marejesho ya viwango linganifu hulipwa kila juma. Katika vikundi vyote vinavyoshirikiana na taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo, kiwango cha kurejesha mikopo katika benki za vijijini kwa wakati kwa mwaka ni asilimia 98 hadi 100.

Viwango vya utendaji na taasisi za fedha za Ghana

Kwa kawaida ni taasisi rasmi za mikopo zinazozingatia viwango vya utendaji kama vile uwiano wa mitaji. Nyingi ya taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo zisizo rasmi au zilizo nusu rasmi hazijaanzisha viwango vya utendaji. Hata hivyo idadi kubwa ya taasisi hizi tayari zimeshatambua umuhimu wa kuzingatia viwango vya utendaji ili kuhakikisha zinakuwa endelevu. Kuhusu tathmini ya athari, baadhi ya taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo hufanya tathmini kila baada ya kipindi fulani ili kuona athari ya shughuli zao kwa wateja wao.

Changamoto kwa taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo

Taasisi zinazotoa mitaji midogo midogo nchini Ghana zinakabiliwa na changamoto kadhaa katika utoaji wa huduma za kifedha unaofaa zaidi kwa watu masikini, hasa wanawake. Changamoto hizi zinahusu masuala ya uchumi mkubwa (uchumi makro), maendeleo ya kitaasisi, na njia za kuzifikia fedha za mikopo. Lakini changamoto nyingine muhimu ni ile ya kuboresha mbinu za kuwafikishia huduma wafanyabiashara masikini wanawake.

*Kwa maelezo zaidi juu ya mada hii tafadhali wasiliaa na: Shimwaayi Muntemba, chumba namba j3 – 101, world bank, 1818 H Street NW, Washington D.C. 20433. Tel. No: (202) 458-7370; e-mail address: smuntemba@worldbank.org

 

[Back to TOC]


Footer