|
AFYA: MAARIFA YA ASILI, FAIDA LINGANIFU na
Katy Moran Mimea
kama madawa Mjadala wa haki za uvumbuzi unaonyesha umuhimu wa
bioanuwai kwa afya ya binadamu. Tangu zama za kale hadi sasa,
mimea imekuwa msingi wa famasia. Spishi kutoka nchi za tropiki
zina utajiri mkubwa wa bioanuwai na biokemikali kutokana, kwa
kiwango fulani, na hali ya hewa ya maeneo hayo. Katika maeneo
yenye halijoto wastani, majira ya baridi kali huwaua wadudu
waharibifu wa mimea, na mimea inayohimili halijoto wastani husitawi
majira ya kuchipua kabla idadi ya wadudu waharibifu wa mimea
haijaongezeka. Lakini kwa vile spishi za tropiki haziathiriwi
sana na wadudu waharibifu wa mimea wa majira mbalimbali, nyingi
zimejitengenezea kinga ya kikemikali dhidi ya wadudu wengi waharibifu
wa mimea. Kemikali hizi za mimea ya tropiki zilizoongeza ustahimilivu
wa mimea hiyo dhidi ya bakteria na vijidudu vingine viharibifu
zinaweza pia kutoa kinga na zikatumiwa kutengenezea dawa kwa
afya ya binadamu. Leo hii, robo ya madawa yetu yanatokana na
mimea. Katika nchi zinazoendelea, asilimia themanini ya wananchi
wake hutegemea mimea kwa matunzo ya afya yao ya msingi. Nchi
Nyingi ya nchi zenye utajiri wa bioanuwai hupatikana
kwenye tropiki za Kusini, ilihali nchi zenye utajiri wa teknolojia,
zenye rasilimali kwa ajili ya maendeleo endelevu ya bioanuwai,
hupatikana zaidi Kaskazini kwenye halijoto wastani. Kabla CBD
haijafungamanisha mataifa na bioanuwai zao, bioanuwai hizo zilichukuliwa
kuwa ni “urithi wa binadamu wote”. Kila mtu aliruhusiwa kutumia
rasilimali za kibiotiki, na zilikuwepo taratibu chache mno za
kisheria za kurejesha faida zilizotokana na uvumbuzi wa madawa
katika nchi zilizo chimbuko la uvumbuzi huo. CBD sasa inajitahidi
kuleta urari wa jinsi wahusika wote wa harakati hizi wanavyoweza
kufaidika na matumizi endelevu ya bioanuwai na viambato vyake.
Nchi za Kaskazini zinaweza kutumia bioanuwai ya nchi za Kusini
kwa kushirikiana teknolojia na faida inayotokana na matumizi
ya kibiashara ya bioanuwai. Ni jukumu la kila nchi mwanachama
wa CBD, hadi sasa ziko nchi 169, kutunga sera ya taifa ya bioanuwai
ikielekeza namna ya utekelezaji
wa suala hili nchini, ikiwa ni pamoja na kutunga sheria za utekelezaji
huo. Baraza la Utafiti wa Kisayansi na Viwanda la India, linalopata
ruzuku kutoka serikalini, kwa mfano, hivi karibuni limeanzisha
programu ya kuzuia uigaji wa uvumbuzi wake ili kulinda mkusanyiko
wa maarifa yake kuhusu madawa yatokanayo na mimea. Makampuni
Tangu CBD ianzishwe, hakuna dawa kutoka nchi za tropiki
iliyotengenezwa kwa maarifa ya kimapokeo inayouzwa kibiashara.
Faida za kiuchumi bado hazijapatikana. Utengenezaji wa dawa
kwa kawaida huhitaji utafiti ghali na wa muda mrefu ili kupata
ithibati ya serikali kabla dawa husika haijaanza kuuzwa. Nchini
Marekani, dawa mpya huchukua, kwa kawaida, miaka 10 hadi 15
kuwa tayari kwa matumizi, baada ya uwekezaji wa zaidi ya $ milioni
300 na kampuni na wawekezaji wanaokubali kuchukua dhima ya kuitengeneza,
kuifanyia majaribio na kuiuza dawa hiyo mpya. Kwa kampuni mpya,
miundombinu kama vile majengo, vifaa na mishahara ya wanasayansi
watafiti lazima vigharamiwe kabla dawa yenyewe haijaanza kuzalisha
mapato. Ili kupata fedha hizi nyingi zinazohitaji kugharamia
utafiti na maendeleo ya madawa, makampuni hutegemea mtaji wa
kijasiri, faida za hisa, ubia na mashirikiano ya namna hiyo
– uwekezaji na watu wa nje katika mradi wa kampuni wenye hatari
nyingi, lakini pia wenye faida kubwa. Wawekezaji waweza kuwa
watu binafsi ama mashirika na uwekezaji wao una hakimiliki ya
ruhusa ya kutengeneza, kuuza, na kutumia madawa yatakayovumbuliwa.
Hakimiliki hutoa kinga ya uvumbuzi kwa kampuni, na hivyo kuwawezesha
wawekezaji kurejesha fedha walizowekeza kwenye utafiti na maendeleo
ya madawa, pale madawa hayo yanapouzwa kibiashara. Hayamkiniki
kwamba kampuni yoyote ama mwekezaji yeyote atahatarisha mtaji
wake kugundua au kuendeleza dawa fulani bila uwekezaji huo kulindwa
kwa hakimiliki dhidi ya ushindani na makampuni mengine. Tamaduni
Asilimia sabini na nne ya madawa
makuu 121 yatokanayo na mimea yana matumizi yanayofanana kwa
tamaduni nyingi za asili. Badala ya kuchagua na kuichunguza
mimea kiholela, mkakati ulio bora zaidi ni kwa baadhi ya makampuni
kutumia maarifa ya asili ili kuitambua miti bora zaidi kwa madawa
mapya. Lakini mikakati michache sana inayojishughulisha na jinsi
maarifa ya asili yanavyoweza kufikiwa na faida linganifu zinavyoweza
kugawanywa kwa kuzingatia utamaduni unaohifadhi mifumo ya kijamii
iliyoujenga. Tofauti kati ya uchumi wa soko, uliokitwa kwa umiliki
wa watu binafsi, na uchumi wa kijumuiya, ambao kwa kawaida huwezesha
kumiliki pamoja rasilimali za kibiolojia na kiutamaduni, humaanisha
kwamba kikundi kizima cha kitamaduni lazima kifaidike. Ni vikundi
vichache sana vya asili vimeshirikishwa katika mijadala ya kitaifa
kuhusu masuala haya, au kuhusu ufafanuzi na utekelezaji wa CBD
katika nchi zao. UCHUNGUZI
KIFANI
Nigeria
Kiutendaji, uchunguzi kifani wa jinsi gani nchi mbalimbali,
makampuni na tamaduni zinaweza kushirikiana na kutekeleza malengo
ya CBD ni ule wa Kampuni ya Madawa ya Shaman (Shaman Pharmaceuticals,
Inc.) ya Nigeria. Kwa mujibu wa daktari Tom Carlson, Mkurugenzi
Mwandamizi wa Utafiti wa Uwandani wa Etinobiotiba wa kampuni
ya Shaman, “Katika nchi hii ya Afrika Magharibi, yenye utajiri
wa bioanuwai na tamaduni, mifumo ya dawa ya asili inasitawi
sambamba na fursa za dawa za Magharibi. Mnamo mwaka 1995, serikali
ya Nigeria iliwaunganisha rasmi waganga wa kienyeji katika huduma
ya afya ya taifa kama watoaji wa matunzo ya afya na leo hii
theluthi mbili ya watoaji wa matunzo ya afya ni waganga wa kienyeji
wa namna moja au nyingine” (Carlson et al., 1997). Nchini Nigeria, Profesa Maurice Iwu ni mwanasayansi
na Mkurugenzi wa Programu ya Maendeleo na Hifadhi ya Rasilimali
za Kibiolojia (Bioresources Development and Conservation Programme
– BDCP), ambalo ni shirika lisilo la kiserikali (NGO) la Nigeria.
Iwu anafafanua, “BDCP ilianzishwa mwaka 1991 kama kitovu cha
mashirikiano ya kitafiti yanayojenga stadi za kiufundi nchini
Nigeria ili kwamba rasilimali za kibiolojia ziwe chombo imara
cha maendeleo endelevu. Stadi zilizoboreshwa zinapelekea kwenye
uchunguzi wa makini zaidi wa madawa ya magonjwa ya kitropiki
yanayopatikana kwa wingi nchini Nigeria kama vile malaria, leishimaniasisi,
na tripanosomiasisi” (Iwu, 1996). Kampuni
ya Madawa ya Shaman
Kampuni ya Madawa ya Shaman ilianzishwa mwaka 1990
na, kupitia BDCP, ikaanzisha ushirikiano wa kitafiti na asasi
za kisayansi za Nigeria, jumuiya za vijijini, na waganga wa
kienyeji na vyama vyao. Kampuni hii ndogo, ambayo makao yake
makuu yako California, ilianza utafiti ukilenga katika uvumbuzi
na uendelezaji wa madawa mapya yanayotokana na mimea yenye historia
ya kutumiwa na wenyeji. Lisa Conte, Rais na mwasisi wa kampuni
anaelezea juu ya suala hili, “Kama jina lake linavyoashiria,
Shaman hutumia sayansi ya etnobotania, na pia kemia ya kutenga
na ya mazao asilia, sayansi ya tiba ya maradhi na famakolojia
ili kupata mbinu bora zaidi ya ugunduzi wa madawa. Wakati ikiundwa
kama kampuni ya kuzalisha faida, Shaman ilianzisha pia Hifadhi
ya Msitu wa Madawa (Healing Forest Conservancy), shirika lisilo
la kutafuta faida lililoanzishwa mahususi kutafuta utaratibu
wa kurejesha faida kwa nchi na tamaduni zinazoshirikiana na
Shaman baada ya madawa kuuzwa kibiashara.” Ingawa kampuni hii
changa bado haijauza madawa yake, matumizi ya etnobotania katika
utafiti yamewezesha dawa zinazotafitiwa na kampuni kuanza kufanyiwa
majaribio ya matumizi mapema sana (King, et al., 1996). Faida
za Moja kwa Moja na za Muda wa Wastani Zilizosambazwa Nchini
Nigeria
Iwu na mwanasayansi mwingine wa Nigeria, Cosmos Obialor,
walipendekeza majadiliano ya awali na waganga na viongozi wa
kimapokeo kuzungumzia juu ya kushirikiana na kampuni ya Shaman
muda mrefu kabla ya kuanzishwa kwa CBD huko Rio mwaka 1992.
“Tulizitembelea jumuiya ambako tulikuwa tumefanya kazi kwa miaka
kadhaa,” alisema Iwu, “ikiwa ni pamoja na vijiji alikozaliwa
Obialor na nilikozaliwa mimi. Kimsingi, kila jumuiya, au kijiji
hujitawala chenyewe kikiwa na chifu na serikali yake. Utaratibu
wao wa kufikia maamuzi ya kijumuiya hujumuisha chifu wa kijiji,
washauri wake, waganga wa kienyeji na wazee,” aliongeza Iwu.
Baada ya majadiliano ya muda mrefu, vikundi hivi viliafiki kwamba
kampuni ya Shaman ilikuwa na malengo kama yao na yaliyozingatia
utamaduni kuhusiana na afya ya binadamu. Kutokana na majadiliano
haya na yale ya awali, sera mwafaka za ushirikiano na kampuni
zilifikiwa. Majadiliano yaliyopelekea kwenye makubaliano yalihusu
maswala kama vile nia na malengo ya mradi; vipi na wapi mimea
itachanganuliwa; fursa ya kibiashara ya mimea hiyo na namna
ya kugawana faida. “Tangu wakati huo, utafiti wa uwandani wa kietnobotania
umeshafanyika mara nne,” alisema Steven King, Makamu wa Rais
Mwandamizi wa Etnobotania na Hifadhi wa Kampuni ya Shaman. “Kwa
uchaguzi wa washirika wa Kinigeria, faida zimechukua umbo la
warsha na programu za mafunzo juu ya afya ya jamii, botania,
hifadhi na etnobotania; msaada kwa hifadhi ya mimea ya dawa;
vifaa kwa ajili ya shule za vijijini; ukusanyaji wa vifaa vya
kibotania kwa ajili ya hebaria (mahali pa kuhifadhia mimea iliyokaushwa);
vifaa vya maabara kwa ajili ya utafiti wa kisayansi wa mimea
inayotibu magonjwa ya vimelea yaliyoenea sana Afrika Magharibi
na kuwasaidia wanasayansi wa Kinigeria ili waweze kutumia mbinu
mpya za uchanganuzi. Kutimiza sera ya kampuni, faida za moja
kwa moja na za muda wa wastani, kama za hapo juu, zenye jumla
ya thamani ya dola za Marekani 200,000 (elfu miambili) zimegawanywa
kupitia katika programu mbalimbali kwa washika dau wanaoshiriki
katika mpango huu”. Iwu aliongeza, “Kampuni hupeleka ripoti za uchunguzi
wa maabarani mara kwa mara kwa jumuiya zinazoshiriki kwenye
mradi. Maandiko ya kawaida kuchapishwa kuhusu mimea ya madawa
kutoka Nigeria yakionyesha utambuzi wa umma wa faida za maarifa
ya kimapokeo ya Nigeria kwa jamii na afya ya binadamu”. Faida
za Muda Mrefu
Baada ya madawa kuuzwsa kibiashara, kampuni ya Shaman
itatoa asilimia fulani ya faida zake kwa Nigeria na makampuni
mengine yaliyoshiriki mradini kupitia kwenye Hifadhi ya Msitu
wa Madawa kwa kipindi chote kampuni itakapokuwa na faida. Hifadhi
itagawa faida hizi, kwa usawa, kwa nchi na tamaduni zote zilizo
washirika na kampuni ya Shaman, bila kujali nchi ama utamaduni
ulio chanzo cha mmea wa dawa au maarifa ya kimapokeo yanayouzwa
kibiashara. Katika mradi kama huu ambapo mapato yake ya kifedha
hayatabiriki, kusambaza faida na hatari za hasara miongoni mwa
washirika wote wa Shaman kunaongeza fursa za fidia (Moran, 1997). Kampuni ya Shaman na Hifadhi zinafuata kanuni ya CBD
kwamba wahifadhi wenyeji wa bioanuwai wanapofaidika kutokana
na matumizi endelevu ya mimea yao ya madawa na watu wengine
wa nje, basi fursa za uhifadhi huongezeka. Ili kuzuia shinikizo
la uchumi mwingine ambao unaweza kuwa na athari mbaya kwa bioanuwai,
faida za kuilinda bioanuwai hiyo lazima zionekane mahali bioanuwai
ilipo. Hata hivyo, kukosekana kwa modeli mwafaka kunafanya nadharia
tete hii isithibitishwe. Ili kujaribu uwezekano wa kutumia mapatano
ya dhamana kama chombo cha kugawana faida, Hifadhi imetoa $
40,000 (dola elfu arobaini) kwa mfuko wa dhamana nchini Nigeria
kwa ajili ya mradi wa majaribio. Mfuko wa Maendeleo Unganifu ya Vijijini na Madawa
ya Kienyeji (Fund for Integrated Rural Development and Traditional
Medicine – FIRD – TM), mfuko huru wa dhamana, ulianzishwa na
BDCP kama chombo cha fedha kwa ajili ya maendeleo endelevu ya
vijijini na kwa ajili ya kusambaza faida miongoni mwa washika
dau wa Nigeria. Bodi ya mfuko huu inajumuisha vikundi vyote
vya washika dau, yaani viongozi wa vyama vya waganga wa kienyeji,
maofisa waandamizi wa serikali, wawakilishi wa mabaraza ya vijiji
ya makabila mbalimbali na wataalam wa kiufundi kutoka kwenye
asasi za kisayansi. Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi wa Mfuko,
Mtukufu Eze E. Njemanze wa 0werri, ni mtawala wa kimapokeo anayeheshimika
sana. Nafasi kubwa inayochukuliwa na mifumo ya mshikamano wa
kimapokeo, kama vile vyama vya kikabila na vyama vya kitaalam
vya waganga, hutoa muundo wa kijamii unaohakikisha ushiriki
wa jumuiya. Vikundi mbalimbali vya kitamaduni vya Nigeria vitapatiwa
fedha kupitia vyama vya waganga wa kienyeji na vijiji kulingana
na desturi zao. Vyama vya mijini, wakuu wa vijiji na vyama vya
kitaalam vya waganga vimepewa uwezo wa kufanya maamuzi kuhusu
miradi ya maeneo yao. Miradi itakayopatiwa fedha itafuata vigezo
vya kusitawisha hifadhi ya bioanuwai na kuendeleza madawa, na
kadhalika usitawi wa kijamii na kiuchumi wa tamaduni za vijijini.
Kwa ngazi ya kijiji, stadi za kiufundi zilizopatikana kutokana
na kugawana faida husaidia kusanifisha na kukuza madawa fita
(phytomedicines), kusambaza na kushirikiana taarifa zinazowafaidisha
waganga wa kienyeji na afya za jumuiya wanazozihudumia. Uzinduzi wa FIRD-TM ulitangazwa jijini Abuja, Nigeria,
kunako Septemba 30, 1997, wakati wa kongamano la kimataifa juu
ya mimea ya madawa lililohudhuriwa na mawaziri watano wa Nigeria
na wakuu kadhaa wa mashirika ya serikali ya Nigeria, ikiwa ni
pamoja na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Hifadhi ya Mazingira
la Shirikisho la Nigeria. Waziri wa Makao Makuu ya Shirikisho
ya Abuja alisema, “… stadi za waganga wa kienyeji ambao pia
ni wahifadhi wa utamaduni wetu wa madawa ya asili sasa zinapatiwa
nafasi yake mwafaka katika jamii”. Dhana ya mfuko wa dhamana inatoa fursa zaidi ya kushawishi
na kusimamia vyanzo vya fedha kutoka NGO nyingine, mashirika
au makampuni yenye wito wa kuchangia katika mfuko ulio imara.
Wakati mchango wa Hifadhi ulipotangazwa, Chama cha Wazalishaji
wa Madawa ya Asili na Kampuni ya Madawa ya 0range za Nigeria
ziliahidi kuchangia fedha zaidi kujaliza mchango wa Hifadhi.
Mwaka ujao, mradi utatathiminiwa na kutumiwa kuiongoza Hifadhi
kuanzisha mfuko wa dhamana wa kiolezo utakaotumiwa na washirika
wote wa kampuni ya Shaman, makampuni na mifuko mingine ya kutoa
misaada. MASUALA YALIYOBAKIA
Uchunguzi kifani wa kampuni ya Shaman nchini Nigeria
unatoa mfano wa jinsi nchi, vikundi vya utamaduni na makampuni
yanavyoweza kushirikiana kwa faida ya washika dau wote kuleta
maendeleo endelevu ya bioanuwai kwa ajili ya afya ya binadamu.
Ni njia mojawapo ya kutimiza malengo ya CBD na kila mshiriki
anapaswa kuendelea kutafuta, kubainisha na kuagiza mbinu mpya
zinazofaa zaidi kwa mazingira yake. Nchi, tamaduni na makampuni
yanayoshirikishwa yametofautiana mno kiasi kwamba hatua zinazochukuliwa
zitafaa tu iwapo zitazingatia miktadha mahususi ya kiutamaduni,
kiuchumi na kimazingira. Masuala yafuatayo bado hayajapatiwa
ufumbuzi. ·
Nigeria
ilitoa mkakati wa ushirikiano kwa ajili ya kampuni ya Shaman,
kwa kushirikisha asasi zenye uwezo kamilifu, hasa kwenye ngazi
ya kijiji. Mifumo hii inayojitegemea, ikiwa na machifu wao na
serikali zinazofanya kazi, ilichagua kutumia maarifa yao ya
kimapokeo kuhusu ulimwengu wa nje kufikia malengo ambayo iliyaona
muhimu kwake. Vikundi mbalimbali vya asili vina imani zinazotofautiana
kuhusu shughuli za biashara na vina mitazamo inayotofautiana
kuhusu dhana ya soko. Tofauti hizi hazipashwi kamwe kuwa kisingizio
cha kuvitenga vikundi vya kiasili na matumizi endelevu ya bioanuwai,
kwani huu ndio uamuzi wao pekee wa kufanya, na sio ufanywe na
NGO zisizo za kiasili, kama inavyofanyika mara nyingi, NGO zinazodai
kuwakilisha mawazo ya wenyeji katika kutoa uamuzi juu ya masuala
haya. ·
Kifungu
8 (j) ni sehemu ya CBD inayozungumzia kuhifadhi na kuheshimu
maarifa ya asili. Lakini kinatoa ulinzi hafifu sana wa vikundi
vya utamaduni na kina- lazimisha CBD ifuate sheria za nchi.
Kisheria, ni washiriki wa CBD, sio sera za makampuni, wenye
mamlaka ya kuamua jinsi ya kutekeleza maendeleo endelevu ya
bioanuwai katika maeneo yao. Hali ya kisiasa ya nchi vinamoishi
vikundi vya kiasili ni muhimu kwa mafanikio ya maendeleo ya
bioanuwai. Kwa vile vikundi vya kiasili ni washika dau wakubwa
wa masuala ya CBD, ni lazima vishirikishwe kwenye mijadala ya
mataifa yao kuhusu ufafanuzi na utekelezaji wa CBD. Ili kuhakikisha
kudumishwa kwa mifumo yao ya kiutamaduni, ni lazima vishiriki
na vipigania vyenyewe masilahi yao. Kama nchi zinataka kufaulu
vema kuhifadhi spishi za dunia, mikakati yao lazima ilenge kuwashirikisha
watunzaji wa bioanuwai, na sio ilazimishwe juu yao kutoka kwenye
ngazi za juu. ·
Kufungamanishwa
kwa wenyeji na maeneo ya kimapokeo kunaongoza matendo yao yanayohusiana
na ikolojia. Utambuzi wa kisheria na serikali wa haki za maeneo
unavipatia mamlaka vikundi vya wenyeji kuwakatalia ama kuwaruhusu
watu wa nje kuingia katika maeneo hayo – hatua ya kwanza ya
kuhifadhi bioanuwai kupitia usimamizi wa kimapokeo wa ardhi
na rasilimali. Lakini suala hili muhimu lilipewa uzito mdogo
sana kwenye warsha ya hivi karibuni ya CBD iliyofanyika Madrid
na kuhudhuriwa na wawakilishi wa serikali na vikundi vya wenyeji.
Watu wengi waliona kuwa hii ilikuwa ni fursa iliyopotezwa. Wengine
waliiona warsha hiyo kama hatua ya kwanza ambako maagizo ya
kimaendeleo kuhusu hifadhi ya bioanuwai kupitia haki za maeneo,
kama vile Sheria Na. 8371 ya Philippines, yangeweza kutangazwa.
Jambo lililobaki ni kuangalia endapo katika mikutano inayofuata
suala la hifadhi ya bioanuwai kupitia haki za maeneo litabanwa
tena na madondoo mengine ya ajenda (Burgiel, et al., 1997). ·
Taarifa
sahihi ni jambo muhimu. Ni wajibu kwa washika dau wote wa CBD
kuwa na uelewa sahihi wa dhana ya haki za uvumbuzi. Haki hizi
si mbadala wa haki za ardhi na haki za binadamu na kukatishwa
tamaa hujitokeza pindi watu wanapojaribu kuzitumia haki za uvumbuzi
kwa malengo yasiyo yake. Jambo litakalofaulu ni kwa nchi, tamaduni
na makampuni kuchangia pamoja uzoefu wao, kwani hakuna mfumo
mmoja pekee unaoweza kufaa katika mazingira yote. Hifadhi na
maendeleo endelevu ya bioanuwai yanahitaji mikabala tofautitofauti. Makala hii imerekebishwa kidogo kutokana na makala
inayoitwa “Moving On: Less Description, More Prescription for
Human Health” iliyoandikwa na Katy Moran, katika Ecoforum, Journal of the Environment
Liaison Center International, Vol. 21, No. 4, Januari 1998.
Kwa taarifa zaidi juu ya somo hili, tafadhali wasiliana na Katy
Moran, Mkurugenzi Mtendaji, Hifadhi ya Msitu wa Madawa, 3521 S Street,
NW-Washington, DC 20007. <Moran HFC@aol.com>
|