THE WORLD BANK GROUP A World Free of Poverty
Home

[Back to TOC]

USITAWISHAJI WA CHAMA CHA KILIMO NCHINI MALI:
KUONGEZA VIWANGO VYA UWEZESHAJI WA WENYEJI

Mwanzoni mwa miaka ya 1980,wanachama wa vyama vya vijijini (associations villageoises,  au kwa kifupi AV) wa Koutiala huko Kusini mwa Mali walikuwa na suala la kutatua na Kampuni ya Nguo ya Mali (Campagnie Malienne des Textiles, CMDT). Uvumi ulikuwa ukienea kwamba CMDT ilikuwa imepanga kuwaongezea malipo wafanyakazi wake wa ugani (yaani mgao wao wa faida kutokana na pamba), bila kuongeza bei waliyolipwa wakulima. Wawakilishi wa vyama mbalimbali vya vijijini tayari walikuwa wameunganisha nguvu zao mwaka 1989 kutaka sera iliyochukuliwa na CMDT kuhusu wajibu wa kifedha wa vyama vya wazalishaji ibatilishwe, matakwa ambayo hatimaye yalikubaliwa.

Wakiwa wametiwa nguvu na ushindi huo wa awali, wawakilishi hawa waliunganisha tena nguvu zao kukabili tatizo la bei na wakaanzisha Kamati ya Uratibu ya Vyama vya Vijijini na “Tons” ya Koutiala, iliyojumuisha wawakilishi wa vyama mbalimbali vya wenyeji. Wajumbe wa Kamati ya Uratibu walijumuisha wakulima waliofuzu kisomo chenye manufaa na wenye uzoefu katika harakati za kupigania masoko zilizokuwa zikiendelea kusini mwa Mali tangu miaka ya 1970,  na pia wawakilishi wachache wa kizazi kipya kilichojitokeza katika muongo uliotangulia: wahitimu wa elimu ya sekondari na vyuo waliokuwa wamerejea kwenye jumuiya zao za asili ili kuanzisha mashamba yao.

Kubadili mfumo wa kiutawala na kisiasa

Mfululizo wa mikutano na vikao ulikiwezesha kikundi kuandaa orodha rasmi ya madai na malalamiko. Wakati huohuo, matukio ya kisiasa yaliyoikumba Mali yalichochea mageuzi makubwa katika vyama vya vijijini, yakipunguza zaidi faida ya mauzo ya pamba na kuilazimisha Kamati ya Uratibu kuchukua hatua. Mnamo mwaka 1991, kikundi kiliamua kumwagiza mjumbe wake msomi kuliko wote, mhitimu wa chuo cha kilimo aliyekuwa amerejea kwenye jumuiya kujiunga na kilimo, azungumze na wanachama wa vyama vya vijijini, awatulize wasiwasi wao na kuwasilisha madai yao kwa CMDT. Jambo hili, lililolengwa kwa AV, lilifanikiwa sana: wawakilishi wa vyama waliiunga mkono kabisa Kamati ya Uratibu. Lakini uongozi wa CMDT, ukiwa na wasiwasi kutokana na hali geugeu ya kisiasa, ulikataa kufanya mapatano yoyote na Kamati hii ya wakulima. Kutokana na hali hii, kamati iliitisha mgomo wa wazalishaji wa pamba, na wanachama wake wakatembelea eneo lote kushawishi AV kuunga mkono mgomo. Kwa miezi miwili, vyama viligoma kupeleka pamba kwenye CMDT, hadi Waziri wa Maendeleo ya Vijijini alipokuja mwenyewe Koutiala kusuluhisha mgogoro huu. Matokeo ya mapatano haya yalikuwa kwamba CMDT ilikubali msingi wa majadiliano ya pamoja juu ya bei ya zao kupitia shirika lisilo la kiserikali lililowakilisha wazalishaji wa pamba. Aidha CMDT ilikubali shirika hilo kushiriki pia kwenye Bodi ya Taifa ya kupanga bei za mazao ya kilimo.

Kwa njia hii, SYCOV (Syndicate des Productears du Coton et du Vivrier au Umoja wa Wazalishaji wa Pamba na Mazao ya Chakula) ilianzishwa, ingawa ilichukua mwaka mmoja zaidi kuanzishwa rasmi kisheria, kutokana na taratibu za kiutawala zilizohitajika kutekelezwa. Uongozi wa Umoja huu mara moja ulifungua milango ili vyama vya vijijini vya Kusini mwa Mali vijiunge na hata ukaamua kuondoa, kwa maridhiano, ugombea wa kiongozi mkuu wa harakati za mwaka 1991, kwa uraisi wa Umoja huu mpya, ili kumwezesha mwakilishi wa mojawapo ya mikoa iliyojiunga kwenye Umoja huu agombee nafasi hiyo. Umoja huu, unaoendesha shughuli zake kwa lugha mbili (Kibambara na Kifaransa), umeendelea kukua, bila kujali baadhi ya vipingamizi vya CMDT na matatizo ya ndani ya Umoja yanayosababishwa na mabadiliko geugeu ya AV, baadhi ya maamuzi tenge ya uongozi na mifarakano kati ya uongozi wa angazi za chini (za vijijini) na wa ngazi za juu. Kwa sasa ni sehemu ya mfumo wa kiutalawa na kisiasa nchini Mali kwamba wakulima wana haki ya kushiriki katika maamuzi yote ynayowahusu. SYCOV pia inandaa mafunzo ya Kifaransa cha kuzungumza na kuandika kwa wawakilishi wa AV wanaofahamu Kibambara tu na tayari inatumia lugha mbili (Kibambara na Kifaransa) katika hati zake zote na katika mikutano yake.

Mizizi ya mabadiliko: kuhamishia nguvu za kiuchumi kwa wenyeji

Kusema kweli, pamoja na nguvu na udhaifu ya SYCOV, majaribio ya Umoja huu tayari  yanawakilisha hatua ya pili ya uwezeshaji wa wenyeji katika vijiji vya Kusini mwa Mali na unaonyesha baadhi ya faida zinazoweza kupatikana  kutokana na kuhamishia mamlaka ya kiuchumi mikononi mwa vyama vya wakulima. Ingawa pamba imekuwa ikilimwa na kuuzwa katika maeneo haya kwa zaidi ya miaka thelathini, hali imebadilika katika kipindi cha miaka kumi na mitano iliyopita, kutoka ile hali ambapo wafanyakazi wa makampuni makubwa kama vile CMDT na washirika wao walidhibiti ununuaji wa mazao vijijini na kuyasafirisha hadi viwandani na kwenda kwenye mfumo ambapo takribani shughuli zote hizi sasa hutekelezwa na mashirika ya vijijini.  Wawakilishi wa vyama hivi vya wenyeji au mashirikisho ya sasa wanashughulikia kikamilifu upimaji wa uzito wa mazao, kuwalipa wakulima, kuhifadhi mazao, kuyasafirisha hadi kwenye viwanda vya usindikaji, na kuyauza tena kwa walaji  na kadhalika kushughulikia mipango na mahesabu na uundaji wa sera za mashirikisho husika. Jambo hili kubwa lilifanikiwa kwa kiwango kikubwa kutokana na programu za kisomo chenye manufaa na elimu isiyo rasmi zilizotekelezwa kwa msaada wa makampuni yenyewe ya pamba (au pengine programu zilizorithiwa toka juhudi za awali za serikali ama za NGO), iliowezesha vijana na watu wazima wenye elimu ndogo kupata stadi za kusoma, kuandika na za kiuhasibu katika lugha zao na kuielewa vema mifumo ya usimamizi katika lugha ya kuzaliwa ama katika lugha mbili (ya kuzaliwa na ya Kifaransa).

Hatutakuwa tunatia chumvi tukisema kuwa juhudi hizi zimeyawezesha makampuni ya pamba kuokoa mabilioni ya faranga (CFA francs, kwa wastani CFA 500=US$ 1). Sehemu ya kutosha ya mapato haya imerejeshwa kwenye vyama vya jumuiya ambavyo navyo vimewagawia wakulima kupitia vipunguo vya bei na kuchangia kwenye mifuko ya pamoja ya uwekezaji. Kwa upande wake, mifuko ya uwekezaji imehamasisha mfululizo wa uwekezaji mwingine kama vile uanzishwaji wa vyama vya kuweka na kukopa fedha, ununuzi wa zana bora zaidi za kilimo, uchimbaji wa visima vipya vya maji, ujenzi wa kliniki na shule za jumuiya, n.k. Hali hii ya udhibiti wa wenyeji ina uhusiano na ongezeko kubwa la uzalishaji wa pamba katika Afrika Kusini mwa jangwa la Sahara kwenye muongo uliopita, jambo ambalo limelipandisha Bara hadi nafasi ya nne kwenye soko la dunia na kuzisheheneza bajeti za kitaifa zilizobanwa sana na masharti ya programu za kurekebisha uchumi wa nchi hizo.

Pamba haiwezi kufikiriwa sana kama kichocheo cha maendeleo endelevu, zikizingatiwa athari zake mbaya kwa rutuba ya udongo, hasa kutokana na mfumo wa mbadilisho mazao na wa hifadhi ya udongo unaotumika huko Afrika Magharibi. Hata hivyo, uzoefu wa pamba umeonyesha, kwa kiwango kikubwa, uwezo wa wazalishaji wa ngazi ya vijijini wa kuendesha wenyewe shughuli za kibiashara na kiusimamizi – mradi wawe wamepatiwa mafunzo yanayohitajika. Pia uzoefu huo imepelekea kuanzishwa asasi imara za vijijini zinzotoa “mifano halisi” ya maendeleo katika nyanja kadhaa nyinginezo.

Muktadha unaofaa: Mwingiliano wa changamoto ya kiuchumi na mtaji wa kijamii.

Vyama vya vijijini kwa kweli  viliibuka kutokana na athari za mambo mawili, moja la “kimapokeo” na jingine la kisasa; na muungano wa mambo haya mawili ndiyo sababu kuu ya matokeo yaliyopo. Kwa kawaida jumuiya za Mali ya  Kusini zimeunganika katika “ton” (kwa lugha ya Kibambara-Kimalinke) au miungano ya namna hii miongoni mwa vikundi vya makabila mengine ya jirani. Vikundi hivi vya marika aghalabu husukwa vizuri sana na vina uongozi imara. Vikundi vya “ton” ndivyo vilivyoshughulikia masuala ya uuzaji na uwekezaji wakati CMDT ilipofanya jaribio lake; na dhima zao mpya ziliwezesha vikundi kubadili mielekeo yake na kuanzisha mifumo ya uwajibikaji na mafunzo iliyokuwa bora zaidi ya ile iliyotekelezwa na vikundi vya jando vya kimapokeo.

Hivyo, kwa maana hii kushindwa, kufaulu na juhudi anzilishi za SYCOV zinawakilisha “safu ya pili” katika kampeni ya kukuza uwezo wa wenyeji na uwezeshaji wa vyama vya vijijini ulioanza kwa urekebishaji upya wa mfumo wa mauzo ya pamba miaka kadhaa iliyopita, na unaondeshwa na miundo iliyopo ya kijamii. Na wakati huohuo juhudi hizi zimesaidia kuendeleza mambo mengineyo.

Kupeleka maendeleo ya wenyeji kwenye safu ya pili

Mfumo mwingine mzuri: ili kuboresha usimamizi wake, vyama vya vijijini vya kusini mwa Mali, vikisaidiana na CMDT na msaada toka nje ya nchi, vilianzisha mnamo mwaka 1993 chombo maalum chenye dhamana ya kukagua mahesabu yao na kutoa msaada wa kiufundi kwa viongozi wenyeji kuhusu masuala  ya kifedha. Chombo hiki kiliitwa “Kituo cha Usimamizi cha Koutiala” (Koutiala Management Center); na tayari kimeshaanzisha matawi yake kadha tangu wakati huo. Kituo kina wafanyakazi kutoka vyama vya vijijini, ambao hutoa huduma ya ukaguzi wa mahesabu kwa AV. Wafanyakazi wenyeji  hupatiwa mafunzo na kisha kusaidiwa kiufundi na wataalam wa nje ya maeneo yao kwa muda kabla hawajajitegemea wenyewe. Sera ya Kituo husimamiwa na Baraza la Uongozi, ambalo kwa upande wake limeunganishwa na Shirikisho la Vyama vya Vijijini vya Mali ya Kusini. Kinadharia, Kituo kinapaswa kuendeshwa kwa bajeti inayolipwa kutokana na mapato ya huduma za Kituo kwa vyama vya vijijini. Hivyo Kituo kiko katika hatua ya kati: baina ya kuwa “kampuni tanzu kamili” ya shirikisho na shirika binafsi la ukaguzi wa mahesabu.

Lakini kwa kweli, Kituo kilianzishwa, na kingali kwa kiwango fulani, kikitegemea msaada wa fedha toka nje. Hata hivyo Kituo kinaonekana kumudu awamu ya kwanza ya uanzishwaji wa uendeshwaji  na kwa hakika kinatoa huduma zinazohitajika pamoja na kuzalisha mapato.

Msingi wa makala hii ni data zilizokusanywa na Peter Easton, Gay Belloncle, Cheibane Coulibaly, Simon Fass, Laouali Malam Moussa na timu tano za utafiti za kitaifa wakati wa Utafiti wa Elimu wa PADLOS kuhusu “Ugatuaji wa Madaraka na Ujenzi wa Uwezo wa W enyej ikatika Afrika Magharibi uliofadhiliwa na Club du Sahe/OECD na CILSS. Kwa ripoti kamili ya utafiti wasiliana na Peter Easton, Center for Policy Studies in Education, 312 STB, College of Education, Florida State University, Tallahassee, FL 32306, USA; simu (850) 644-1595;e-mail: easton@coe.fsu.edu

 

 

[Back to TOC]


Footer