THE WORLD BANK GROUP A World Free of Poverty
Home

[Back to TOC]

WAENDESHA BENKI ZA VIJIJI: UZOEFU WA FANDENE (SENEGAL)

 Fandene, kijiji cha Waserere na Wawolof kilichopo kilomita sita kutoka Thies, Senegal, kwenye eneo la nchi linalolimwa karanga, ni makao makuu ya shirika la kuweka na kukopa fedha lenye mafanikio makubwa. Shirika hilo sasa linajumuisha vijiji 34  katika eneo lote,  lina mtaji wa zaidi ya faranga (CFA) milioni thelathini (takribani $ 60,000) na limeshatoa zaidi ya mikopo 1,500 kwa wakazi wa jumuiya za eneo hilo. Chanzo cha shirika hili zilikuwa ni harakati za wenyeji kupambana na matatizo ya ukame na kupungua kwa rutuba ya mashambani yaliyoikumba Senegal yote ya kati.

Fandene yenyewe ni matokeo ya maingiliano ya kihistoria kati ya mbari za Kiserere na Kiwolof. Kijiji hiki kwa kiwango kikubwa ni cha Kikristo na kwa miaka mingi kilikaliwa na wamisionari wa Kikatoliki na kuwa kituo kikuu cha jumuiya, lakini huchangia rasilimali chache za bonde la jirani na kingo za msimu za mto na jumuiya za Kiislam kadhaa mbalimbali. Hatua za hivi karibuni zilizochukuliwa na wenyeji kwa kiwango fulani zinatokana na mtazamo wa wahamiaji kutoka Fandene dhidi ya kiwewe cha ukame mkuu wa Saheli cha mwanzoni mwa miaka ya 1970. Katika juhudi za kuwasaidia wanajumuiya wa nyumbani kwao kupata ufumbuzi wa tatizo lililokuwa linawakabili na kukwepa jumuiya isitoweke, vijana waliokuwa wamekwenda kusoma shule ama kufanya kazi, walishiriki kuunda Chama cha Vijana wa Fandene (“Association des Jeunes de Fandene – AJF) mnamo mwaka 1972.

Kutoka Utamaduni hadi Kilimo

Kwa miaka kumi na mitano ya kwanza ya uhai wake, AJF ilijishughulisha zaidi na kufadhili matukio ya kiutamaduni yaliyolenga kuwahamasisha vijana waikumbatie ama wairejelee jumuiya yao ya nyumbani, na wakati huohuo warejeshewe utambulisho wao wa kiutamaduni. Miradi ya maendeleo ilipewa uzito mdogo, lakini hata hivyo shughuli za AJF ziliwafanya baadhi ya wasomi vijana kurejea kuishi kijijini tena na hivyo kuunda kikundi kipya cha wakulima wa “kisasa” na wenye mtazamo wa kihakiki. Polepole kikundi hiki hakikuridhika na programu ya AJF kujibana na matukio ya kiutamaduni tu na kuongozwa na watu wa kutoka nje.

Hivyo, kunako mwaka 1987, Chama kilichukua msimamo mpya. Katika kukabiliana na upungufu wa muda mrefu wa chakula eneoni, wanachama wa AJF walianza kufanya utafiti wakishirikiana na wanajumuiya za jirani ili kulielewa vema zaidi tatizo lao na kulipatia ufumbuzi unaowezekana. Utafiti huu ulikuwa na matokeo matatu muhimu:

·         Watafiti waliabaini kuwa hatua kadhaa zilikuwa tayari zimeanza kuchukuliwa na wakulima wadogowadogo wenyewe – hatua zilizokuwa na nafasi kubwa ya kupanua uchumi wa wenyeji wa kuboresha msingi wa maliasili, lakini hatua ambazo zilikuwa zikikwamishwa na upungufu wa mikopo na mitaji ya kuiendeleza.

·         Ukosefu wa huduma za mikopo kwa kiasi kikubwa ulitokana na ukosefu wa dhamana za mikopo na chombo ambacho kingewadhamini wakulima wadogowadogo.

·         Wakati huohuo, wanachama wa AJF walichunguza hali na utendaji kazi wa miradi ya hivi karibuni ya eneoni iliyokuwa ikifadhiliwa na mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs), na kubaini kuwa mingi ya miradi hiyo haikufanikiwa kwa vile ilibuniwa nje na haikuendana na juhudi zilizopo za wananchi.

Kutatua tatizo la mikopo

Uamuzi ulikuwa kukabiliana na matatizo haya kwa kuanzisha namna fulani ya chombo cha kuweka na kukopa fedha kisicho rasmi. Mwanzo ulikuwa wa kiwango cha chini: kila mwanachama wa AJF alichangia FCFA 250 (takribani $ 1 ya wakati huo) kwenye mfuko wa pamoja na mfuko huo ukaanza kutoa mikopo midogomidogo kwa wanakijiji kwenye miradi inayofaa. Wakopaji walilipa riba ya asilimia 15 kwa mwaka, huku wakitafuta njia nyingine za kuongeza mitaji yao. Mojawapo ya njia hizo ilikuwa kupanua uanachama wa mfuko hadi kwa jumuiya za jirani. Kazi hii haikuwa ngumu. Vijiji vya jirani viliihitaji sana huduma hii na hivyo vyenyewe vilikuwa na shauku kubwa ya kutaka kujiunga na mfuko.

Kwa njia hii, mtandao wa ushirika wa kuweka na kukopa fedha polepole ulisambaa kwenye jumuiya zote 34 za eneo la Fandene na kuwa na muundo imara zaidi. Kila tawi la ushirika – jumla ya matawi 19 – lilikuwa na kitengo cha wanawake na kitengo cha wanaume, na viongozi wa kila kitengo walipatiwa mafunzo ya uhasibu, kutathmini thamani ya mikopo na uendeshaji wa mikopo. Wakazi wa jumuiya zilizochangia kwenye mfuko walishawishiwa kuomba mikopo kwa maandishi kupitia maofisa wao wa vitengo, na uongozi wa ushirika polepole ulijifunza kufanya upembuzi yakinifu wa mikopo iliyoombwa na kuwapatia wakopaji msaada wa kiufundi katika kuhakikisha kuwa mikopo yao ingelipishika. Hatimaye timu ya watathmini iliundwa ili kuzisaidia kamati za wenyeji za kuweka na kukopa fedha kujifunza mbinu za kutathmini maombi ya mikopo na za kukabiliana na mahitaji ya kiufundi ya wafanyabiashara wadogowadogo.

Kusaidia uvumbuzi mpya wa kiuchumi wa wenyeji

Ushirika uliopanuka zaidi wa kuweka na kukopa fedha uliwekea mkazo maalum katika kuwasaidia wakulima na wafanya biashara ndogondogo kuvumbua mikabala mipya ya kuimarisha kilimo na uuzaji wa mazao yao. Ifuatayo ni mifano ya mambo yaliyotekelezwa na ushirika katika miaka mitano ya kwanza ya uhai wake:

·         Vikundi vya uzalishaji vya wanawake vilisaidiwa kubuni mbinu za uuzaji bidhaa zilizowakwepa walanguzi, na hivyo kuwawezesha wanawake kuuza matunda-mwitu (“bissap fruits”) kutoka misitu ya jirani na vikapu vya kienyeji moja kwa moja kwenye soko la Dakar na pia kwenye vyama vingine vya vijiji eneoni. Hadi kufikia mwaka 1995 vikapu elfu moja vilizalishwa kila wiki kwa mtindo huu.

·         Chama cha AJF kilitoa mikopo kwa wakulima waliotaka kurejesha tena kilimo na mauzo ya mihogo eneoni na waliotaka kupanua upandaji na matumizi ya kunde.

·         Mikopo ilitolewa kwa vikundi vya wanawake ili kuanzisha ushirika wa utengenezaji sabuni na mauzo yake.

·         Mashirika ya kuweka na kukopa fedha yalitoa mikopo mingi kwa ajili ya kuchimba visima, uendelezaji wa bustani za kumwagilia na uuzaji wa mazao ya bustani hizo.

Kadiri shughuli na mtaji vilivyoongezeka, ndivyo ukubwa na idadi ya mikopo vilivyoongezeka pia. Kwa kipindi cha miaka mitano ya kwanza, wastani wa matumizi ya fedha katika sekta mbalimbali ulikuwa kama ifuatavyo:

     Maendeleo ya mifugo na soko lake                                 FCFA 5,600,000

     Viwanda na biashara ndogondogo                        -            FCFA 2,800,000

     Kilimo bora                                                      -            FCFA   500,000

     Uchimbaji visima                                               -            FCFA    500,000

Faida za mwaka kutokana na uendeshaji wa mikopo zilipanda pia kutoka chini ya FCFA 100,000 mwaka 1991 hadi kufikia zaidi ya 700,000 kunako mwaka 1994 na ilipofikia mwaka 1998 mtaji wa chama cha kuweka na kukopa fedha kilichounganisha vijiji kadhaa pamoja uliongezeka hadi kufikia zaidi ya FCFA milioni 30,  au  takribani $ 60,000.

Kusuka mfumo mpya wa kijamii na kiuchumi

Hata hivyo, matokeo  yaliyokuwa muhimu zaidi ya shughuli hizi ni ujenzi wa ushirika na muunganisho wa jumuiya za Kisenegal zenye mbari (makabila) zinazotofautiana. Vijiji 34 vya Fandene vinajumuisha Wakristo, Waislamu na waumini wa dini za kienyeji na vina mchanganyiko wa makabila (Waserere, Wawolof, Wabambara, Wafulani…). Lakini licha ya mchanganyiko huu, watu hawa wameshirikiana vema kuanzisha vyombo vya kuweka na kukopa fedha na pia katika kuviendesha. Vitengo vya wanawake na wanaume vya chama cha AJF daima vimekuwa na nguvu na uzito ulio sawa.

Licha ya hayo, chama kimeanzisha mipango ya uuzaji wa mazao na vyama vya ushirika vya wakulima wadogowadogo katika maeneo mengine ya Senegal ambako bidhaa nyingi za wanachama huuzwa huku nao wakinunua mahitaji yao kutoka kwa wakulima hao. Jambo muhimu zaidi ni kwamba chama cha Fandene kimeanzisha timu za kiufundi ili kuvisaidia vikundi vichanga na visivyo na uwezo wa kifedha vya jirani na jiji la Thies na mji mkuu wa taifa, Dakar, ambavyo vinahitaji kuanzisha programu zao za kuweka na kukopa fedha. Kwa hali hii msaada wa kiufundi sasa unatoka vijijini na kupelekwa mijini!

 

[Back to TOC]


Footer