Wanawake wa Senegal Wajenga Upya Utammaduni
Wao
Kwa
miongo mingi makao makuu ya Utawala wa Kifaransa huko Afrika Magharibi,
yaani nchi ya Senegal, kama zilivyo nchi nyingine za Sahel, wakazi
wake wengi wanaendelea kuishi vijijini. Ingawa asilimia 62 ya watu
huishi vijijini, hata hivyo zaidi ya asilimia 85 ya utajiri wa nchi
iko mijini. Kama ilivyo kwa nchi nyingi, wanawake na wasichana ndio
walio katika hali ngumu zaidi. Mwaka 1995, kiwango cha kujua kusoma
na kuandika cha wanawake kitaifa kilikuwa karibu nusu ya kile cha
wanaume (asilimia 23 ikilinganishwa na asilimia 44), na tofauti ilikuwa
kubwa zaidi huko vijijini. TOSTAN,
inayomaanisha “kujitoa kutoka katika yai” katika Kiwolof, lugha inayozungumzwa
na idadi kubwa zaidi ya wananchi milioni 7.9 wa Senegal, ni miongoni
mwa mipango kadhaa ya kielimu ya maendeleo ya vijijini na ya wanawake
inayoshughulikia matatizo kwenye machimbuko yake. Mpango hutoa programu
ya mafunzo ya miezi 18 inayojumuisha elimu ya msingi kwa lugha za
kitaifa inayozingatia masuala halisi ya kimaendeleo, na huwapatia
wanavijiji rasilimali za kuboresha hali zao za maisha huku wakizidi
kujiamini katika kukabiliana na maisha yao. Licha ya kujua kusoma
na kuandika, programu hii kamambe huwapatia washiriki zana za kushughulikia
masuala ya kijamii kama vile afya, usafi wa mazingira. Mpango
hutumia viunzi sita vinavyounganisha ujuzi wa kusoma na kuandika na
stadi za maisha katika utaratibu shirikishi wa kutatua matatizo. TOSTAN
imefaulu kuendeleza mfungamano kati ya elimu ya msingi na maendeleo
ya vijijini, ikiwapatia watu wazima wanaosoma sio tu ujuzi na kusoma,
kuandika na kuhesabu katika lugha zao za kitaifa, bali mbinu za kuyaelewa
na kuyatatua matatizo yao. Miaka
kadhaa iliyopita, shirika lisilo la kiserikali la TOSTAN liliitikia
maombi ya viongozi wa kijiji cha Malicounda ambao walikuwa wameshaona
athari za programu zake za mafunzo kwa wanawake katika jumuiya za
jirani na kuisaidia jumuiya hii ya Wabambara wa Senegal ya Kati Magharibi
kuanzisha kituo chake. Programu ilitilia mkazo maalum juu ya utambuaji
na utatuzi wa matatizo ya kawaida, na kimoja kati ya viunzi vya mwisho
vya mafunzo kilishughulikia suala la afya ya wanawake na ngono. Programu
hii ilivunja rekodi kwa kuungwa mkono mno na wanawake wa vijijini.
Mara tu baada ya kumaliza mafunzo yao, wanawake waliojua kusoma na
kuandika wa Malicounda waliamua kulishughulikia suala la kijadi la
tohara ya wanawake – utamaduni wa siku nyingi wa jumuiya za Wabambara/
Wamandigue na Wapulaar. Wakitumia uzoefu wa maeneo mengine na athari
za tohara kwa afya ya wasichana na maisha yao ya kingono, waliandaa
hoja nyingi ambazo hatimaye zililifanya baraza la kijiji kufuta rasmi
desturi ya kufanya tohara. Wakati wa miezi ya Mei hadi Julai 1997
– kipindi cha kawaida cha kutahiri wasichana wadogo – tohara hazikufanyika
Malicounda kwa mara ya kwanza katika historia ya jumuiya hiyo. TOSTAN
na UNICEF ziliwaunga mkono wanawake kwa kuandaa ziara ya waandishi
wa habari ishirini wa Kisenegal waliowatembelea na kuwauliza maswali
juu ya msimamo wao. Wanawake waliwafanyia wageni wao igizo kuwaonyesha
sababu za kufikia uamuzi huo na hoja walizozitumia kuwashawishi wanakijiji
wengine. Ziara hii ililitangaza sana suala hili, lakini pia ilizua
maoni ya vitisho na kukosolewa kutoka jumuiya jirani za kabila la
Malicounda. Wakiwa wamehuzunika lakini bila kutishika, wanawake wa
kikundi cha Malicounda waliamua
kuandaa ujumbe kwenda kwenye vijiji viwili vya jirani kuwashawishi
wanawake wa huko juu ya umuhimu wa uamuzi wao wa kukomesha ukeketaji
wa viungo vya kike. Katika
moja ya jumuiya hizo – jumuiya ya Wangerin Bambara – wanawake waliohitimu
punde tu programu ya TOSTAN waliamua kukiidhinisha “kiapo cha Malicounda”.
Rais wa Chama chao cha wanawake, mwenyewe binti wa ngariba, alisema
kwamba binti yake alitokwa na damu nyingi sana alipotahiriwa, na hivyo
wakati wa kubadili mila hii ulikuwa umewadia. Wakazi
wa jumuiya ya pili, Waker Simbara, walimua kwamba wasingeweza kuifuta
mila hii bila kushauriana na wanakabila wenzao wa vijiji vya jirani.
Hivyo kwa kipindi cha majuma manane, wanaume wawili ambao walikwisha
shiriki katika programu za TOSTAN – mmoja mwezeshaji wa TOSTAN na
mwingine Imam wa Msikiti mwenye umri wa miaka 66 (kiongozi mwandamizi
wa Kiislam) – walizuru kijiji kimoja baada ya kingine kujadili na
wananchi madhara ya tohara kwa wanawake. Awali wanaume hawa walidhani
kuwa wangefukuzwa katika jumuiya nyingi. Badala yake waligundua kuwa
taarifa za Malicounda zilifungua milango na nyoyo, na wakasikia maelezo
ya kutisha toka kwa wanawake, wakielezea kwa mara ya kwanza juu ya
uzoefu wao. Wanaume
hawa wawili walirejea wakiwa wameshawishika juu ya umuhimu wa kile
walichosikia na kile walichokuwa wakikifanya. Waliwasaidia wanawake
wa Malicounda, Ngerin na Ker Simbara kuandaa mkutano wa vijiji vyote
huko Diabougou. Mnamo Februari 1998, wawakilishi watatu – chifu wa
kijiji na wawakilishi wawili wa kike – kutoka vijiji kumi na vitatu
walikutana kwa siku mbili kujadili tatizo la tohara na wakaunda “Azimio
la Diabougou”, lililowataka wanavijiji 8,000 kusimamisha mara moja
tohara kwa wasichana. Taarifa
za mkutano huu zililifikia eneo la Casamance la Senegal ya Kusini,
ambako kikundi kingine cha vijiji – vyote vya Wapulaar, kabila linalotahiri
asilimia 88 ya wasichana – kilifanya mkutanno na maazimio kama yale
ya Diabougou. Mkutano wao ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka jumuiya
18, na wafanyakazi wa sekta ya afya na Imam aliyeheshimika sana wa
Medina Cherif, aliyewahakikishia wanawake kwamba dini ya Kiislamu
haihitaji wasichana watahiriwe na inawahakikishia wanawake haki ya
afya na hadhi ya utu. Wanawake wengi walielezea madhara yanayoletwa
na tohara. Mmoja alieleza kwa masikitiko juu ya vifo vya binti zake
wawili waliopoteza maisha baada ya kutahiriwa; na ngariba alikiri
kuwa kuna msichana aliyekufa kijijini kwake mwaka jana. Wanawake wengine
walizungumzia juu ya matatizo wakati wa kujifungua na juu ya maumivu
wakati wa kujamiana. Kikundi kilihitimisha mkutano wake kwa kutoa
azimio lililokana tohara. Mpango
huu umeendelea kupanuka. Mapema ulipoanza, Rais Abdou Diouf wa Senegal
mwenyewe alipendekeza “ Kiapo cha Malicounda” uwe mfano wa kuigwa
na taifa zima. Mara tu baada ya mikutano ya Casamance, wanawake wa
eneo la St. Louis la Senegal wanaandaa sasa mkutano wa vijiji vyao,
utakaofanyika Februari 1999. Utaratibu
wa “ Mafunzo tendaji” unaoendeshwa miongoni mwa wanawake na mpango
wa TOSTAN nchini Senegal unaelekea kuleta mabadiliko makubwa ya kiutamaduni.
Mambo yanayochangia kwenye mafanikio ya mpango wa TOSTAN wa elimu
na maendeleo endelevu yanajadiliwa zaidi hapa nchini. Hoja MIZIZI
YA UTAMADUNI. Pamoja na utumiaji wa lugha za kitaifa, kuthamini kwa
kiwango kikubwa utamaduni wa Kiafrika ndio msingi wa mpango wa elimu
wa TOSTAN, unaoonyesha mfungamano wa kiutendaji baina ya utamaduni
na elimu. LUGHA
ZA KITAIFA.Ingawa Kifaransa ndio lugha rasmi ya Senegal, serikali
imezidi kuhimiza matumizi ya lugha za kitaifa katika programu za kujifunza
kusoma na kuandika, kwa vile inatambua kuwa mafunzo huwa mepesi zaidi
mtu anapotumia lugha yake ya kuzaliwa. Aidha uelewa wa lugha ya kuzaliwa
huweza kuwa ni msingi mzuri wa kujifunza lugha za kimataifa. Kujifunza
kwa kutumia lugha ya kuzaliwa huleta heshima na fahari, huwapa wanawake
uwezo wa kuelezea mambo yao majumbani mwao na katika jumuiya zao;
huwafanya watu wajivunie mahali waishipo, na hivyo kuwapa moyo wanaume
kuwekeza mitaji kwenye jumuiya yao badala ya kuhamia mijini. Hali
kadhalika, huondoa hali ya kutengwa vijijini wanayihisi watoto walioelimishwa
kwa Kifaransa tu, na hivyo kuleta mawasiliano na mshikamano miongoni
mwa wanachi wa marika mbalimbali. Mhimili
wa programu ni UTATUZI WA MATATIZO, na kutoa motisha kubwa ya kujifunza
kusoma na kuandika. Stadi zinazofundishwa kwenye programu hii yenye
hatua tano ni pamoja na (i) utambuzi na uchambuzi wa tatizo; (ii)
kuchunguza masuluhisho ya tatizo kwa kuzingatia fedha, vifaa, nguvukazi
na muda uliopo; (iii) kupanga suluhisho: kipi kinahitaji kutimizwa?
Ni lini hatua zinapaswa kukamilika? Nani mwenye dhamana ya kufanya
hivyo? Nguvukazi ipi , vifaa gani, na fedha kiasi gani zinahitajika?
Vipingamizi gani vyaweza kujitokeza? (iv) utekelezaji wa suluhisho;
na (v) tathmini ya matokeo: Je, tumelitatua tatizo? USHIRIKI.
Mpango wa TOSTAN ulibuniwa na wanavijiji ukiwashirikisha kwa kiwango
cha juu kabisa kwa kipindi cha miaka kumi. Msingi wa mitaala ya mafunzo
ni hadithi, methali, nyimbo na mila za kila mahali zilizokusanywa
kwa kutembelea kila kijiji na kusikiliza na kurekodi mapokeo simulizi.
Mbinu za kufundishia ni shirikishi na mara nyingi wanafunzi huzishirikisha
familia zao na jumuiya katika harakati za kutatua matatizo. WANAWAKE.
Wanawake ndio wenye kiwango cha chini kabisa cha elimu nchini Senegal,
kiwango chao cha kujua kusoma na kuanduka kikiwa ni asilimia 74.9
mwaka 1990. Wanawake hususan wamekuwa wakifaidika sana na mkabala
wa lugha kamili wa TOSTAN ambao huanza na uzoefu halisi wa maisha
ya kawaida ya kila siku badala ya udhahania. TOSTAN kimekuwa kituo
cha mafunzo ya viongozi kwani wanawake wanapata kujiamini, wanaanza
kutambua matatizo kama vile ya upatikanaji wa maji, na waanza kuleta
mabadiliko katika jumuiya zao. Pamoja na hayo, wanaume hawajatengwa:
takribani theluthi moja ya washiriki ni wanaume, na – kama mfano wa
Ker Simbara unavyoonyesha – wanaweza kuchukua hatua nyingi muhimu
za kupunguza kero zinazowakabili wanawake. Namna
ya kuandaa Mikabala
Licha
ya njia ya ushirikishwaji iliyotajwa awali, wanafunzi pia walihusishwa
katika uandaaji wa maudhui ya programu kwa kutumia mbinu ya majaribio,
mazungumzo na uangalizi wa jinsi maazimio yalivyotekelezwa. Mwanzoni
njia hii ilikuwa ya gharama kubwa lakini hatimaye ilionekana kuwa
ni ya nafuu kutokana na kuigwa kwa mafanikio na mashirika mengine
yasiyo ya kiserikali (NGO). Brosha ya UNESCO kuhusu TOSTAN inaeleza
kuwa elimu ya msingi “hukumbusha mengi katika maisha ya watu kuliko
mradi wa kawaida wa mafunzo ya kusoma na kuandika…. Uelewa wa jinsi
kila kiunzi kitakavyochangia kubadili maisha na mazingira yao ni motisha
yenye nguvu sana kwa wanafunzi”. Namna ya utatuzi wa matatizo ndio
msingi wa mkabala wa TOSTAN na huweza kurekebishwa kwa urahisi katika
mazingira tofauti tofauti. Matatizo
Yaliyokuwepo
Mwaka
1987 hapakuwepo na programu zozote za elimu ya msingi katika lugha
za kitaifa nchini Senegal, na Wizara mbili za serikali zilishughulikia
mafunzo ya kusoma na kuandika lakini aghalabu bila ya mafanikio. Programu
zilizokuwepo zilihusiana kidogo sana na maisha halisi na zilipelekwa
kwa watu wasiojua kusoma na kuandika, ambako stadi zilizofundishwa
na kutotumika kihalisi zilisahaulika baada ya muda mfupi. Programu
ya elimu ya msingi ya TOSTAN ilishughulikia tatizo jingine la msingi,
uchoshi, kwa kuhusisha elimu na maisha binafsi
na ya jumuiya na kuandaa vifaa vya mafunzo vinavyovutia vinavyotokana
na mazingira ya wanafunzi – lengwa. Awali kupata wawezeshaji wa programu
haikuwa rahisi, na washiriki hawakupenda kulipia gharama za wawezeshaji
wao wenyewe. Walipendelea kutumia fedha zao kugharamia vifaa vya mafunzo
au ujenzi wa madarasa. Wahitimu wa TOSTAN ndio sasa wamepatiwa mafunzo
ya kuwa wawezeshaji na ndio wanaofanya idadi kubwa ya wafanyakazi
wa TOSTAN. Masuluhisho
na Mahitimisho
Stadi
za kutatua matatizo zinazotolewa kwenye kiunzi cha kwanza ndizo hutumiwa
kwenye viunzi vyote vingine, vinavyoshughulikia: mambo ya usafi, uongezaji
maji chumvi mwilini na chanjo, stadi za usimamizi wa fedha na vifaa,
usimamizi wa nguvukazi, uchunguzi wa hali halisi na miradi ya kuzalisha
mapato. Kwa kutumia stadi hizi, washiriki wanawake wameanzisha miradi
kadha midogo midogo ya uzalishaji mali. Mbinu za TOSTAN vilevile zimetumika
kuwanufaisha watoto walioko nje ya shule kwa kuwaandalia mtaala unaojumuisha
kusoma, kuandika, hesabu, utatuzi wa matatizo, afya na usafi, lishe,
uongozi wa familia, haki za watoto, historia, jiografia, elimu ya
amani, stadi za uongozi na dinamiki (nguvu) za vikundi. Kwa kutumia
mkabala shirikishi, vijana (watoto waliobalehe) hujifunza kutoa matini
zao wenyewe. Kipeperushi
cha UNESCO kuhusu TOSTAN kimetoa hitimisho linalofaa: “kuwepo kwa
programu kamambe inayowapatia washiriki zana za kutatua matatizo na
inayoshughulikia matatizo muhimu ya afya, usafi, na mazingira ni jambo
lenye manufaa kwa maeneo mengi ya Afrika yanayokabiliwa na viwango
vikubwa vya ujinga, hasa miongoni mwa wanawake. Mkazo zaidi wapaswa
kuwekwa juu ya utekelezaji wa programu hizi zilizochunguzwa na kujaribiwa
vema badala ya kubuni programu mpya… TOSTAN imeonyesha kuwa watu wasio
na elimu yoyote rasmi, kutoka vijiji vyenye rasilimali chache kabisa,
wanaweza kuboresha maisha na mazingira yao kupitia programu imara,
na hivyo kuwa huru na kujitegemea zaidi”. *Msingi wa makala hii ni utafiti uliofanywa na watafiti wa Senegal kwa
msaada na ushauri wa kiufundi wa Prof. Peter Easton wa Chuo Kikuu
cha Jimbo la Florida, wakishirikiana na baadhi ya jumuiya za Kiafrika.
Utafiti ulifadhiliwa na Club du Sahel/OECD, CILSS na ADEA.
|