THE WORLD BANK GROUP A World Free of Poverty
Home

[Back to TOC]

Uvumbuzi upya wa Uanagenzi na Taratibu za Kuingia Utu Uzima: Kuingia kwenye Uchumi – miji katika Afrika Kusini mwa Sahara

Jamii nyingi za kimapokeo katika Afrika Kusini mwa Sahara zina mifumo mizuri ya kuwaingiza vijana katika desturi, stadi na uelewa wa utu  uzima. Mifumo hiyo hujumuisha vyama vya marika, unyago na jando, na uanagenzi katika stadi mbalimbali za uzalishaji mali.

Utaratibu wa kimapokeo kwa ajili ya uanagenzi na jando na unyago bado una mashiko katika jumuiya za vijiji ilihali unalegalega kwenye maeneo ya pembezoni mwa miji miongoni mwa watu ambao njaa, ukosefu wa ajira au mvuto wa maisha mazuri zaidi umewafanya wakimbilie mijini. Hapana shaka kuna mambo mbalimbali yanayounganisha maeneo haya mawili, na vyama vya wahamiaji kutoka vijiji na mikoa mbalimbali ni mambo ya kawaida mijini.

Kizazi Kilichoachwa Kifanye Kipendavyo

Kwa ujumla, uhamiaji mijini kutoka vijijini umechangia katika kuvunja polepole uhusiano na nguvu za mila za jando na unyago na utaratibu wa uanagenzi tangu upatikane “uhuru wa bendera”. Mfano wa upeo wa uvunjaji wa desturi hizi za kuingia utu uzima pengine unaonyeshwa na hali ya watoto wa mitaani, wale vijana wasio na elimu, kazi na aghalabu makazi ya kudumu ambao wanazurura katika barabara kuu na ndogo za miji ya Afrika.

Mashirika ya Umoja wa Mataifa na ‘NGO’ nyingi zinazoshughulikia suala hili huwachukulia watoto wa mitaani kama kikundi cha watoto wanaofanya kazi – yaani, watoto wadogo ambao hawajafikia umri rasmi wa kuajiriwa au hawajakomaa kijamii ambao wanafanya kazi katika mazingira yenye kuleta madhara katika makuzi na maendeleo yao. Watoto wengi katika jamii zinazoendelea, ni kweli, kuwa wanafanya kazi na wataendelea kufanya kazi.

Changamoto iliyo sahihi zaidi sio kukataza aina zote za kazi kwa watoto wenye umri mdogo, bali kuhakikisha kwamba watoto hawalazimishwi kufanya kazi zisizofaa na za hatari kwa sababu ya kuokoa maisha yao, na kwamba wapatiwe fursa nzuri za kuingia katika maisha ya utu uzima.

Lakini hali mbaya ya watoto wa mitaani inadokeza hali ya uchumi ilivyo pembezoni mwa miji, ambako ukosefu wa fursa za kijamii umewanyima vijana wakimbizi nafasi ya kukuza utambulisho wa utu uzima. Miundo ya kimapokeo ya jamii si rahisi kujitokeza sasa. Kama methali ya Kihausa inayosema “In rawa ta sake, ki’di ita ma sai ta sake”: Mdundo wa ngoma unapobadilika, uchezaji wa ngoma pia hubadilika. Ipi ni midundo mipya ya maana katika mazingira ya sasa ya kiuchumi na kiutamaduni, na kadhalika hali iliyobadilika inayoitia changamoto midundo hiyo? Mifano mitatu kutoka Afrika na mmoja kutoka Caribbean inatoa mwangaza kwa kiasi fulani.

Kusimamisha wimbi la watoto wa mitaani: Chama cha Undugu cha Kenya

Chama cha Undugu kilianzishwa kwa juhudi za padri mmoja wa Kiholanzi aliyehamia Nairobi mwaka 1972 baada ya uzoefu wa miaka 17 ya kuishi vijijini nchini Tanzania, ambako alianzisha huduma za kichungaji kwa vijana wa mijini. Vijana wachache waliziitikia programu zake za kidini, lakini aliona kwamba mitaa ya Nairobi ilifurika vijana wasio na ajira, hasa vijana “waegeshaji magari” ambao waliomba ujira kidogo kutoka kwa wenye magari kwa ajili ya kuyalinda na kuyaosha magari hayo katikati ya jiji la Nairobi lenye msongamano wa watu na vitu.

Mwaka 1973, padri alianza kutumia muda wake mwingi mitaani akijenga uhusiano mwema na watoto wa mitaani na kuzungumza nao kuhusu hali halisi ya maisha yao na juu ya matarajio yao. Aligundua kuwa wengi wao walikuwa wameacha shule za msingi na kuhama toka nyumbani kwao kwa sababu familia zao hazikuweza kuwalipia karo za shule na kuwanunulia sare na vifaa vinginevyo vya shule. Wengi wao, kama kiongozi mmoja wa Chama cha Undugu anavyoeleza, walipoulizwa wanahitaji nini, walijibu “Nataka kusoma”.

Kutokana na sababu hizi, awali padri aliamua kwamba jitihada za kuwasaidia watoto wa mitaani zielekezwe zaidi katika kuwarejesha shuleni, na akaanza kutafuta fedha za kulipia karo na vifaa vingine vya shule kwa vijana wengi kadiri ilivyowezekana. Hata hivyo, aligundua punde kuwa mara nyingi wakuu wa shule waliwakataa watoto hao au hawakutaka warejee kwenye shule zao za awali. Wakuu hao walihofu kuwa sababu zilezile zilizowafanya watoto hawa watoroke shule mara ya kwanza zinaweza zikajirudia; ama kutokana na tabia zilizojengwa huko mitaani, watoto hawa hawawezi kuendana na utaratibu wa kawaida wa shule.

Namna ya kujifunza

Matatizo haya ya kwanza yalifuatiwa na mikakati mbalimbali ambayo hatimaye ilikiwezesha Chama cha Undugu kubuni mkabala wenye mafanikio zaidi uliokidhi hali ya vijana masikini wa Nairobi. Mkabala huo ulikuwa na hatua nne. Hatua ya kwanza ilikuwa mtandao wa “shule zisizo rasmi” zilizoenezwa katika makazi ya watu masikini ndani na pembezoni mwa jiji la Nairobi. Shule hizi zililenga wavulana na wasichana wenye umri wa miaka 10 – 16 ambao walikuwa hawajaenda shule kabisa ama ambao walishindwa kuendelea na shule, na hivyo kuwa katika hatari ya kuwa watoto wa mitaani wafanyakazi, kama kweli walikuwa hawajawa hivyo tayari. Programu hii ilipangwa ichukue miaka mitatu, iwapatie washiriki elimu ya msingi (kusoma na kuandika) na stadi za kunusuru maisha, pia iwawezeshe kujithamini, na hali kadhalika iwawezeshe wale wanaohitaji kurudi kwenye utaratibu rasmi wa elimu au kujiunga na vyuo vya ufundi stadi.

Kurejea huku kwenye elimu rasmi au mafunzo ya ufundi stadi ndiyo ilikuwa hatua ya pili ya mkabala na ilichukua mwaka mmoja zaidi. Wale waliobaki kwenye programu hii – au wale waliorejea baada ya kumaliza shule rasmi – walipata nafasi ya kujaribu ujuzi wao katika kazi mashuhuri za ufundi za sekta ya uchumi isiyo rasmi za Nairobi: hususani ufundi seremala, ushonaji, ufundi magari na ufundi chuma. Kwa kazi zote hizi Chama cha Undugu kilikuwa na zana za kutosha za kufanyia kazi kwenye karakana yake.

Kutafuta nafasi katika jamii

Hatua ya tatu ilijumuisha kipindi cha mpito kuelekea katika ajira na majukumu ya kiuchumi ya utu uzima. Vijana walioonyesha upendeleo wa kazi ya ufundi mahususi walisaidiwa kumpata fundi stadi katika sekta isiyo rasmi ambaye angewachukua kama wanagenzi kwa kipindi cha mwaka mmoja ili wapate mafunzo zaidi na uzoefu. Chama cha Undugu kilishiriki kama mwenzi katika mapatano haya na kikabuni vigezo vya kuteua mafundi stadi “ wenyeji” na taratibu za ukaguzi wa mara kwa mara wa vifaa vya Chama ili kuhakikisha kuwa wanagenzi wanafundishwa  na kwamba mazingira na masharti ya kazi si ya kinyonyaji. Wakati wa mwaka huu wa uanagenzi, vijana walirejea kwenye karakana za Makao Makuu ya Undugu kila juma ili “kuinua viwango vya stadi zao”. Mafunzo haya yalihusu hasa matumizi ya zana za kazi ambazo mafundi stadi wengi hawakuweza kuyafundisha, na wakati huo huo yalilenga kuwatayarisha vijana kufanya mitihani ya kwanza ya serikali ya ufundi stadi kwenye stadi walizochagua. Mitihani hii ilifanyika mwishoni mwa mwaka.

Kuwapatia nafasi za kazi wahitimu wa Undugu, au kuwawezesha kujiajiri wenyewe kwa faida kwenye sekta isiyo rasmi ndiyo ilikuwa hatua ya mwisho na ya nne. Kitengo cha Ushauri wa Kibiashara cha Undugu hutoa mafunzo ya kuanzisha miradi midogo midogo na mikopo kwa wahitimu wa programu ili kuwasaidia wajiimarishe kwenye kazi zao. Chama vilevile kimeanzisha Idara ya Usanifu na uuzaji wa bidhaa na huduma zinazotolewa na sekta isiyo rasmi na hasa katika kazi za ufundi zinazosaidiwa na Undugu na zinazofanywa na mafundi stadi walio na wanagenzi wa Undugu. Wafanyakazi wa Kitengo cha Usanifu Viwanda huendesha warsha kwa mafundi stadi wa sekta isiyo rasmi wanaoshirikiana na Undugu juu ya usanifu na uuzaji wa mazao yao. Kwa kufanya hivyo huwatumia wanagenzi wa Undugu kama nyenzo ya kuboresha mazao yanayotolewa na sekta isiyo rasmi.

Mikabala Mingine Mbalimbali

Huduma ya Uchukuzi ya Watoto wa Mitaani mjini Khartoum

Mkabala tofauti lakini unaohusiana (na ule wa Nairobi) umechukuliwa na shirika lisilo la kiserikali (NGO) – Shirika la Kimataifa la Watoto wa Mitaani (SKWM) linalofanya kazi Khartoum, Sudan (kwa lugha ya kiingereza shirika hili huitwa Street Kids International – SKI). Tatizo la jinsi ya kuwaingiza vijana hawa katika jamii ya mjini na uchumi wa mjini liliwafanya watumishi wa shirika pamoja na vijana wenyewe kutafakari juu ya “unafuu wa kiuchumi” walionao watoto wa mitaani katika soko la mjini. Moja ya stadi zao ni kwamba wanaifahamu vema mitaa – yaani, barabara kuu na ndogo za jiji unganifu la Khartoum, na pia wanaweza kufanya kazi kwa ufanisi katika mazingira ambayo yangewatisha watu wengine. Watumishi na watoto wa mitaani walizingatia ukweli huu dhidi ya kile wachumi wanachokiita sasa “mambo magumu” katika uchumi wa mijini, na hususani ugumu wa kusafirisha vifurushi na vifaa vinginevyo kutoka sehemu moja hadi nyingine ya jiji la Khartoum lenye msongamano wa magari. Ndipo wakaja na wazo la kuanzisha Huduma ya Uchukuzi ya Watoto wa Mitaani.

Mpango huu ulijumuisha mambo yafuatayo:

·         Kukopa baiskeli kwa wachukuzi, ambapo baadaye kila mtoto angelipia mkopo huo kutokana na ujira wake wa kazi.

·         Kuwafunza watoto taratibu za uchukuzi na hatua za usalama.

·         Kuwasaidia kuanzisha mpangilio mzuri wa ufanyaji kazi na utunzaji wa mahesabu utakaoufanya mradi utekelezeke.

Kwa hakika mradi ulikuwa na mafanikio ya kutosha; na mfano wake uliigwa na Shirika la Kimataifa la Watoto wa Mitaani la Banglore, nchini India, miaka michache baadaye.

Chama cha Mafundi Stadi cha Senegal (ENDA/GRAF)

Programu zilizosaidiwa na ENDA (Environment and Development = Mazingira na Maendeleo) katika jiji la Dakar, Senegal, zilianza, kwa namna fulani, kinyume na utaratibu. Watumishi wa ENDA walikuwa wakiwasaidia mafundi stadi wa sekta isiyo rasmi – katika ufundi seremala, utengenezaji vinywaji – kuunda vyama vyao ili kuinua teknolojia yao na kutatua matatizo yao ya ugavi na soko. Hata hivyo, kila shughuli ilianza baada ya kufanya “upelelezi” wa kutosha wa mazingira halisi. Ni utaratibu wa ENDA, na hasa wa kitengo chake cha utafiti (Groupe recherche – action – formation – GRAF), kutumia utafiti unaowashirikisha wanufaikaji kama msingi wa kazi zote za maendeleo katika makazi ya watu masikini ya mijini. Moja ya mambo muhimu waliloliona mafundi stadi kutokana na utafiti huu ni hali ya vijana wengi walioacha shule na kuzurura mijini.

Kutokana na hali hii, vyama viliamua kuanzisha mfumo wake wa uanagenzi ili kuwawezesha vijana wajuane katika sehemu zao za kazi na waingie vizuri kwenye maisha ya utu uzima. Ushirika wa maseremala ndio ulikuwa msitari wa mbele kabisa katika suala hili na ulibuni mfumo wa kuwazungusha vijana walioacha shule na kuchukuliwa kama wanagenzi wa Ushirika kwa mafundi stadi mbalimbali ambako walijifunza stadi za kazi tofautitofauti, na kisha – kwa msaada wa ENDA/GRAF – wakafundishwa pia utunzaji fedha na uongozi wa miradi midogomidogo.

SERVOL nchini Trinidad. Mfano wa mwisho unachukuliwa mahali palipo mbali kabisa na bara la Afrika, lakini panafungamana na bara hilo kwa njia nyingi za kihistoria na kiutamaduni: yaani kisiwa cha Trinidad huko West Indies. Matatizo ya mpito wa vijana kuelekea ukubwani katika mazingira ya mijini ni makubwa kama vile ilivyoonekana kwenye mifano mitatu tulioijadili hivi punde – na kwa namna fulani, chanzo cha programu mashuhuri inayoshughulikia matatizo hayo, SERVOL (Service Volunteered for All” – Huduma Inayoletwa Bure kwa Wote) kimefanana pia. Kama Chama cha Undugu, SERVOL ilianzishwa na padri wa Kikatoliki aliyechukizwa na hali duni ya vijana mjini.  Kama Undugu, SERVOL kimekuwa chama ambacho sio tu kinatoa ajira bali pia hutoa njia mbadala za vijana kufahamiana wanapoingia katika maisha ya utu uzima. Miongoni mwa njia hizo ni “Vituo vya Maisha” vya SERVOL.

Kama jina linavyoashiria, Vituo vya Maisha ni zaidi ya kuwa fursa za kufunzia ufundi stadi. Kwanza kabisa vituo hivi hujengwa na vijana wakubwa ili kupata majengo ya karakana, madarasa na huduma nyingine za kijumuiya. Pia kila kituo hutumika kama kituo cha chekechea, na washiriki wote hupangiwa majukumu ya kuwaangalia watoto wadogo au chekechea hao. Kisha mkazo pia huwekewa ushauri nasaha wa marika na kutoa fursa kwa vijana kueleza matatizo yao ya kijamii na yanayotokana na jazba za ujana huku wakizingatia maadili ya dini kuu tatu za kisiwani mwao: Ukristo, Uislamu na Uhindu. Vijana hushiriki katika kuandaa mtaala wao maalum unaojumuisha uelewa wa kiroho, kimwili, kiakili, kiutamaduni na kimhemko. Kutoka hapo, washiriki huweza kuingia kwenye vyuo vya ufundi stadi na kuajiriwa au kuwa na sifa za kupatiwa mikopo midogo ya kuanzishia miradi yao binafsi. Kiwango cha vijana wanaoshindwa kuendelea na programu hii ni asilimia 5 tu, ambapo kiwango cha kuajiriwa au kujiajiri baada ya kufuzu mafunzo ya stadi mbalimbali ni asilimia 75.

Viambato muhimu:ajira, maana na kujiongoza

Mifano yote hii inawakilisha juhudi za kujaza pengo katika kuwatayarisha vijana wanagenzi masikini waliopoteza utamaduni wao wa kimapokeo na kutupwa kwenye hekaheka za majiji ya Afrika ili waweze kumudu vema majukumu yao ya kiutu uzima. Na mifano hii inaelekea kufaulu vizuri pale inapoyafufua upya mapokeo hayo, huku ikichanganya taratibu za kimapokeo za uanagenzi na za vyama vya marika na mwelekeo mpya wa kiuchumi na kujiongoza na kujitathimini zaidi kwa washiriki.

Mafundisho mengine machache yanajitokeza kutokana na juhudi za kuwasaidia vijana masikini wa Afrika kujenga utambulisho mpya:

·         Mkabala wa “elimu ya watu wazima” hufanikiwa vizuri iwapo utajengwa juu ya uzoefu na stadi walizonazo tayari vijana na kuwapatia nafasi ya kuchangia kutoa maamuzi ya kuendesha programu husika.

·         Ajira yenye faida ni msingi wa utambulisho mpya, lakini sio wa mshikamano. Mshikamano huletwa na kuwepo kwa mpango wa maendeleo wa muda mrefu mbele – uwe wa kidini, kiutamaduni ama kisiasa – na fursa ya kuutumia katika maisha ya mtu binafsi. Hivyo ushauri nasaha wa marika mara nyingi ni jambo muhimu la kufanikisha programu.

·         Namna za kimapokeo za uanagenzi na vyama vya vijana zafaa zitumike kama rasilimali za kusonga mbele kimaendeleo, pia lazima zihakikiwe. Programu za namna hiyo huwa kama uwanja wa majaribio kwa tamaduni nyingi za jirani.

·         Utambuzi wa mazingira yanayomzunguka mtu – na haja ya kuyabadili – ni vijalizo muhimu vya juhudi zozote zile.

*msingi wa makala hii ni utafiti uliofanywa na watafiti wenyeji kwa msaada na ushauri wa kiufundi wa Prof. Peter Easton wa Chuo Kikuu cha Jimbo la Florida, wakishirikiana na baadhi ya jumuiya za Kiafrika. Utafiti ulifadhiliwa na Club du Sahel/OECD, CLISS na ADEA.

Uvumbuzi upya wa Uanagenzi na Taratibu za Kuingia Utu Uzima: Kuingia kwenye Uchumi – miji katika Afrika Kusini mwa Sahara

Jamii nyingi za kimapokeo katika Afrika Kusini mwa Sahara zina mifumo mizuri ya kuwaingiza vijana katika desturi, stadi na uelewa wa utu  uzima. Mifumo hiyo hujumuisha vyama vya marika, unyago na jando, na uanagenzi katika stadi mbalimbali za uzalishaji mali.

Utaratibu wa kimapokeo kwa ajili ya uanagenzi na jando na unyago bado una mashiko katika jumuiya za vijiji ilihali unalegalega kwenye maeneo ya pembezoni mwa miji miongoni mwa watu ambao njaa, ukosefu wa ajira au mvuto wa maisha mazuri zaidi umewafanya wakimbilie mijini. Hapana shaka kuna mambo mbalimbali yanayounganisha maeneo haya mawili, na vyama vya wahamiaji kutoka vijiji na mikoa mbalimbali ni mambo ya kawaida mijini.

Kizazi Kilichoachwa Kifanye Kipendavyo

Kwa ujumla, uhamiaji mijini kutoka vijijini umechangia katika kuvunja polepole uhusiano na nguvu za mila za jando na unyago na utaratibu wa uanagenzi tangu upatikane “uhuru wa bendera”. Mfano wa upeo wa uvunjaji wa desturi hizi za kuingia utu uzima pengine unaonyeshwa na hali ya watoto wa mitaani, wale vijana wasio na elimu, kazi na aghalabu makazi ya kudumu ambao wanazurura katika barabara kuu na ndogo za miji ya Afrika.

Mashirika ya Umoja wa Mataifa na ‘NGO’ nyingi zinazoshughulikia suala hili huwachukulia watoto wa mitaani kama kikundi cha watoto wanaofanya kazi – yaani, watoto wadogo ambao hawajafikia umri rasmi wa kuajiriwa au hawajakomaa kijamii ambao wanafanya kazi katika mazingira yenye kuleta madhara katika makuzi na maendeleo yao. Watoto wengi katika jamii zinazoendelea, ni kweli, kuwa wanafanya kazi na wataendelea kufanya kazi.

Changamoto iliyo sahihi zaidi sio kukataza aina zote za kazi kwa watoto wenye umri mdogo, bali kuhakikisha kwamba watoto hawalazimishwi kufanya kazi zisizofaa na za hatari kwa sababu ya kuokoa maisha yao, na kwamba wapatiwe fursa nzuri za kuingia katika maisha ya utu uzima.

Lakini hali mbaya ya watoto wa mitaani inadokeza hali ya uchumi ilivyo pembezoni mwa miji, ambako ukosefu wa fursa za kijamii umewanyima vijana wakimbizi nafasi ya kukuza utambulisho wa utu uzima. Miundo ya kimapokeo ya jamii si rahisi kujitokeza sasa. Kama methali ya Kihausa inayosema “In rawa ta sake, ki’di ita ma sai ta sake”: Mdundo wa ngoma unapobadilika, uchezaji wa ngoma pia hubadilika. Ipi ni midundo mipya ya maana katika mazingira ya sasa ya kiuchumi na kiutamaduni, na kadhalika hali iliyobadilika inayoitia changamoto midundo hiyo? Mifano mitatu kutoka Afrika na mmoja kutoka Caribbean inatoa mwangaza kwa kiasi fulani.

Kusimamisha wimbi la watoto wa mitaani: Chama cha Undugu cha Kenya

Chama cha Undugu kilianzishwa kwa juhudi za padri mmoja wa Kiholanzi aliyehamia Nairobi mwaka 1972 baada ya uzoefu wa miaka 17 ya kuishi vijijini nchini Tanzania, ambako alianzisha huduma za kichungaji kwa vijana wa mijini. Vijana wachache waliziitikia programu zake za kidini, lakini aliona kwamba mitaa ya Nairobi ilifurika vijana wasio na ajira, hasa vijana “waegeshaji magari” ambao waliomba ujira kidogo kutoka kwa wenye magari kwa ajili ya kuyalinda na kuyaosha magari hayo katikati ya jiji la Nairobi lenye msongamano wa watu na vitu.

Mwaka 1973, padri alianza kutumia muda wake mwingi mitaani akijenga uhusiano mwema na watoto wa mitaani na kuzungumza nao kuhusu hali halisi ya maisha yao na juu ya matarajio yao. Aligundua kuwa wengi wao walikuwa wameacha shule za msingi na kuhama toka nyumbani kwao kwa sababu familia zao hazikuweza kuwalipia karo za shule na kuwanunulia sare na vifaa vinginevyo vya shule. Wengi wao, kama kiongozi mmoja wa Chama cha Undugu anavyoeleza, walipoulizwa wanahitaji nini, walijibu “Nataka kusoma”.

Kutokana na sababu hizi, awali padri aliamua kwamba jitihada za kuwasaidia watoto wa mitaani zielekezwe zaidi katika kuwarejesha shuleni, na akaanza kutafuta fedha za kulipia karo na vifaa vingine vya shule kwa vijana wengi kadiri ilivyowezekana. Hata hivyo, aligundua punde kuwa mara nyingi wakuu wa shule waliwakataa watoto hao au hawakutaka warejee kwenye shule zao za awali. Wakuu hao walihofu kuwa sababu zilezile zilizowafanya watoto hawa watoroke shule mara ya kwanza zinaweza zikajirudia; ama kutokana na tabia zilizojengwa huko mitaani, watoto hawa hawawezi kuendana na utaratibu wa kawaida wa shule.

Namna ya kujifunza

Matatizo haya ya kwanza yalifuatiwa na mikakati mbalimbali ambayo hatimaye ilikiwezesha Chama cha Undugu kubuni mkabala wenye mafanikio zaidi uliokidhi hali ya vijana masikini wa Nairobi. Mkabala huo ulikuwa na hatua nne. Hatua ya kwanza ilikuwa mtandao wa “shule zisizo rasmi” zilizoenezwa katika makazi ya watu masikini ndani na pembezoni mwa jiji la Nairobi. Shule hizi zililenga wavulana na wasichana wenye umri wa miaka 10 – 16 ambao walikuwa hawajaenda shule kabisa ama ambao walishindwa kuendelea na shule, na hivyo kuwa katika hatari ya kuwa watoto wa mitaani wafanyakazi, kama kweli walikuwa hawajawa hivyo tayari. Programu hii ilipangwa ichukue miaka mitatu, iwapatie washiriki elimu ya msingi (kusoma na kuandika) na stadi za kunusuru maisha, pia iwawezeshe kujithamini, na hali kadhalika iwawezeshe wale wanaohitaji kurudi kwenye utaratibu rasmi wa elimu au kujiunga na vyuo vya ufundi stadi.

Kurejea huku kwenye elimu rasmi au mafunzo ya ufundi stadi ndiyo ilikuwa hatua ya pili ya mkabala na ilichukua mwaka mmoja zaidi. Wale waliobaki kwenye programu hii – au wale waliorejea baada ya kumaliza shule rasmi – walipata nafasi ya kujaribu ujuzi wao katika kazi mashuhuri za ufundi za sekta ya uchumi isiyo rasmi za Nairobi: hususani ufundi seremala, ushonaji, ufundi magari na ufundi chuma. Kwa kazi zote hizi Chama cha Undugu kilikuwa na zana za kutosha za kufanyia kazi kwenye karakana yake.

Kutafuta nafasi katika jamii

Hatua ya tatu ilijumuisha kipindi cha mpito kuelekea katika ajira na majukumu ya kiuchumi ya utu uzima. Vijana walioonyesha upendeleo wa kazi ya ufundi mahususi walisaidiwa kumpata fundi stadi katika sekta isiyo rasmi ambaye angewachukua kama wanagenzi kwa kipindi cha mwaka mmoja ili wapate mafunzo zaidi na uzoefu. Chama cha Undugu kilishiriki kama mwenzi katika mapatano haya na kikabuni vigezo vya kuteua mafundi stadi “ wenyeji” na taratibu za ukaguzi wa mara kwa mara wa vifaa vya Chama ili kuhakikisha kuwa wanagenzi wanafundishwa  na kwamba mazingira na masharti ya kazi si ya kinyonyaji. Wakati wa mwaka huu wa uanagenzi, vijana walirejea kwenye karakana za Makao Makuu ya Undugu kila juma ili “kuinua viwango vya stadi zao”. Mafunzo haya yalihusu hasa matumizi ya zana za kazi ambazo mafundi stadi wengi hawakuweza kuyafundisha, na wakati huo huo yalilenga kuwatayarisha vijana kufanya mitihani ya kwanza ya serikali ya ufundi stadi kwenye stadi walizochagua. Mitihani hii ilifanyika mwishoni mwa mwaka.

Kuwapatia nafasi za kazi wahitimu wa Undugu, au kuwawezesha kujiajiri wenyewe kwa faida kwenye sekta isiyo rasmi ndiyo ilikuwa hatua ya mwisho na ya nne. Kitengo cha Ushauri wa Kibiashara cha Undugu hutoa mafunzo ya kuanzisha miradi midogo midogo na mikopo kwa wahitimu wa programu ili kuwasaidia wajiimarishe kwenye kazi zao. Chama vilevile kimeanzisha Idara ya Usanifu na uuzaji wa bidhaa na huduma zinazotolewa na sekta isiyo rasmi na hasa katika kazi za ufundi zinazosaidiwa na Undugu na zinazofanywa na mafundi stadi walio na wanagenzi wa Undugu. Wafanyakazi wa Kitengo cha Usanifu Viwanda huendesha warsha kwa mafundi stadi wa sekta isiyo rasmi wanaoshirikiana na Undugu juu ya usanifu na uuzaji wa mazao yao. Kwa kufanya hivyo huwatumia wanagenzi wa Undugu kama nyenzo ya kuboresha mazao yanayotolewa na sekta isiyo rasmi.

Mikabala Mingine Mbalimbali

Huduma ya Uchukuzi ya Watoto wa Mitaani mjini Khartoum

Mkabala tofauti lakini unaohusiana (na ule wa Nairobi) umechukuliwa na shirika lisilo la kiserikali (NGO) – Shirika la Kimataifa la Watoto wa Mitaani (SKWM) linalofanya kazi Khartoum, Sudan (kwa lugha ya kiingereza shirika hili huitwa Street Kids International – SKI). Tatizo la jinsi ya kuwaingiza vijana hawa katika jamii ya mjini na uchumi wa mjini liliwafanya watumishi wa shirika pamoja na vijana wenyewe kutafakari juu ya “unafuu wa kiuchumi” walionao watoto wa mitaani katika soko la mjini. Moja ya stadi zao ni kwamba wanaifahamu vema mitaa – yaani, barabara kuu na ndogo za jiji unganifu la Khartoum, na pia wanaweza kufanya kazi kwa ufanisi katika mazingira ambayo yangewatisha watu wengine. Watumishi na watoto wa mitaani walizingatia ukweli huu dhidi ya kile wachumi wanachokiita sasa “mambo magumu” katika uchumi wa mijini, na hususani ugumu wa kusafirisha vifurushi na vifaa vinginevyo kutoka sehemu moja hadi nyingine ya jiji la Khartoum lenye msongamano wa magari. Ndipo wakaja na wazo la kuanzisha Huduma ya Uchukuzi ya Watoto wa Mitaani.

Mpango huu ulijumuisha mambo yafuatayo:

·         Kukopa baiskeli kwa wachukuzi, ambapo baadaye kila mtoto angelipia mkopo huo kutokana na ujira wake wa kazi.

·         Kuwafunza watoto taratibu za uchukuzi na hatua za usalama.

·         Kuwasaidia kuanzisha mpangilio mzuri wa ufanyaji kazi na utunzaji wa mahesabu utakaoufanya mradi utekelezeke.

Kwa hakika mradi ulikuwa na mafanikio ya kutosha; na mfano wake uliigwa na Shirika la Kimataifa la Watoto wa Mitaani la Banglore, nchini India, miaka michache baadaye.

Chama cha Mafundi Stadi cha Senegal (ENDA/GRAF)

Programu zilizosaidiwa na ENDA (Environment and Development = Mazingira na Maendeleo) katika jiji la Dakar, Senegal, zilianza, kwa namna fulani, kinyume na utaratibu. Watumishi wa ENDA walikuwa wakiwasaidia mafundi stadi wa sekta isiyo rasmi – katika ufundi seremala, utengenezaji vinywaji – kuunda vyama vyao ili kuinua teknolojia yao na kutatua matatizo yao ya ugavi na soko. Hata hivyo, kila shughuli ilianza baada ya kufanya “upelelezi” wa kutosha wa mazingira halisi. Ni utaratibu wa ENDA, na hasa wa kitengo chake cha utafiti (Groupe recherche – action – formation – GRAF), kutumia utafiti unaowashirikisha wanufaikaji kama msingi wa kazi zote za maendeleo katika makazi ya watu masikini ya mijini. Moja ya mambo muhimu waliloliona mafundi stadi kutokana na utafiti huu ni hali ya vijana wengi walioacha shule na kuzurura mijini.

Kutokana na hali hii, vyama viliamua kuanzisha mfumo wake wa uanagenzi ili kuwawezesha vijana wajuane katika sehemu zao za kazi na waingie vizuri kwenye maisha ya utu uzima. Ushirika wa maseremala ndio ulikuwa msitari wa mbele kabisa katika suala hili na ulibuni mfumo wa kuwazungusha vijana walioacha shule na kuchukuliwa kama wanagenzi wa Ushirika kwa mafundi stadi mbalimbali ambako walijifunza stadi za kazi tofautitofauti, na kisha – kwa msaada wa ENDA/GRAF – wakafundishwa pia utunzaji fedha na uongozi wa miradi midogomidogo.

SERVOL nchini Trinidad. Mfano wa mwisho unachukuliwa mahali palipo mbali kabisa na bara la Afrika, lakini panafungamana na bara hilo kwa njia nyingi za kihistoria na kiutamaduni: yaani kisiwa cha Trinidad huko West Indies. Matatizo ya mpito wa vijana kuelekea ukubwani katika mazingira ya mijini ni makubwa kama vile ilivyoonekana kwenye mifano mitatu tulioijadili hivi punde – na kwa namna fulani, chanzo cha programu mashuhuri inayoshughulikia matatizo hayo, SERVOL (Service Volunteered for All” – Huduma Inayoletwa Bure kwa Wote) kimefanana pia. Kama Chama cha Undugu, SERVOL ilianzishwa na padri wa Kikatoliki aliyechukizwa na hali duni ya vijana mjini.  Kama Undugu, SERVOL kimekuwa chama ambacho sio tu kinatoa ajira bali pia hutoa njia mbadala za vijana kufahamiana wanapoingia katika maisha ya utu uzima. Miongoni mwa njia hizo ni “Vituo vya Maisha” vya SERVOL.

Kama jina linavyoashiria, Vituo vya Maisha ni zaidi ya kuwa fursa za kufunzia ufundi stadi. Kwanza kabisa vituo hivi hujengwa na vijana wakubwa ili kupata majengo ya karakana, madarasa na huduma nyingine za kijumuiya. Pia kila kituo hutumika kama kituo cha chekechea, na washiriki wote hupangiwa majukumu ya kuwaangalia watoto wadogo au chekechea hao. Kisha mkazo pia huwekewa ushauri nasaha wa marika na kutoa fursa kwa vijana kueleza matatizo yao ya kijamii na yanayotokana na jazba za ujana huku wakizingatia maadili ya dini kuu tatu za kisiwani mwao: Ukristo, Uislamu na Uhindu. Vijana hushiriki katika kuandaa mtaala wao maalum unaojumuisha uelewa wa kiroho, kimwili, kiakili, kiutamaduni na kimhemko. Kutoka hapo, washiriki huweza kuingia kwenye vyuo vya ufundi stadi na kuajiriwa au kuwa na sifa za kupatiwa mikopo midogo ya kuanzishia miradi yao binafsi. Kiwango cha vijana wanaoshindwa kuendelea na programu hii ni asilimia 5 tu, ambapo kiwango cha kuajiriwa au kujiajiri baada ya kufuzu mafunzo ya stadi mbalimbali ni asilimia 75.

Viambato muhimu:ajira, maana na kujiongoza

Mifano yote hii inawakilisha juhudi za kujaza pengo katika kuwatayarisha vijana wanagenzi masikini waliopoteza utamaduni wao wa kimapokeo na kutupwa kwenye hekaheka za majiji ya Afrika ili waweze kumudu vema majukumu yao ya kiutu uzima. Na mifano hii inaelekea kufaulu vizuri pale inapoyafufua upya mapokeo hayo, huku ikichanganya taratibu za kimapokeo za uanagenzi na za vyama vya marika na mwelekeo mpya wa kiuchumi na kujiongoza na kujitathimini zaidi kwa washiriki.

Mafundisho mengine machache yanajitokeza kutokana na juhudi za kuwasaidia vijana masikini wa Afrika kujenga utambulisho mpya:

·         Mkabala wa “elimu ya watu wazima” hufanikiwa vizuri iwapo utajengwa juu ya uzoefu na stadi walizonazo tayari vijana na kuwapatia nafasi ya kuchangia kutoa maamuzi ya kuendesha programu husika.

·         Ajira yenye faida ni msingi wa utambulisho mpya, lakini sio wa mshikamano. Mshikamano huletwa na kuwepo kwa mpango wa maendeleo wa muda mrefu mbele – uwe wa kidini, kiutamaduni ama kisiasa – na fursa ya kuutumia katika maisha ya mtu binafsi. Hivyo ushauri nasaha wa marika mara nyingi ni jambo muhimu la kufanikisha programu.

·         Namna za kimapokeo za uanagenzi na vyama vya vijana zafaa zitumike kama rasilimali za kusonga mbele kimaendeleo, pia lazima zihakikiwe. Programu za namna hiyo huwa kama uwanja wa majaribio kwa tamaduni nyingi za jirani.

·         Utambuzi wa mazingira yanayomzunguka mtu – na haja ya kuyabadili – ni vijalizo muhimu vya juhudi zozote zile.

*msingi wa makala hii ni utafiti uliofanywa na watafiti wenyeji kwa msaada na ushauri wa kiufundi wa Prof. Peter Easton wa Chuo Kikuu cha Jimbo la Florida, wakishirikiana na baadhi ya jumuiya za Kiafrika. Utafiti ulifadhiliwa na Club du Sahel/OECD, CLISS na ADEA.

 

[Back to TOC]


Footer