|
MIFUMO YA MAARIFA YA ASILI ENDELEVU KATIKA KILIMO KWENYE MAENEO YA VIJIJINI YA MAJIMBO YA KASKAZINI NA KUSINI YA MATABELELAND NCHINI ZIMBABWE Uchunguzi
Kifani wa Zimbabwe Utafiti
huu ulichunguza Mifumo ya Maarifa ya Asili katika kilimo kwenye maeneo
ya vijijini ya nchini Zimbabwe, ukilenga hasa katika kilimo cha mimea
cha Watonga wa Wilaya ya Binga ya Jimbo la Kaskazini la Matabeleland,
na ufugaji wa kabila la Wakalanga la Wilaya ya Plumtree katika Jimbo
la Kusini la Matabeleland. Utafiti ulilenga kubaini baadhi ya maarifa
ya asili yaliyotumiwa na watu kuhimili maisha katika mazingira magumu
ya hali ya hewa na ya maumbile ya nchi. Malengo
mahususi katika Wilaya zote mbili za Binga na Plumtree yalikuwa: (i)
kubaini athari za kijamii, kisiasa, kidini, kiuchumi na kimazingira za
mifumo ya maarifa ya asili katika kilimo; (ii) kubaini na kuchambua
mbinu za menejimenti (usimamizi) ya maliasili; na (iii) kutathmini
thamani na upungufu wa mifumo ya maarifa ya asili katika kilimo. Mbinu
za Utafiti Taarifa
zilikusanywa kupitia mapitio ya machapisho mbalimbali ya kitaaluma
yanayohusiana na mada, mahojiano na wakulima, kutembelea maeneo ya
kilimo, majadiliano katika vikundi na matumizi ya watafiti walioko
vijijini. Watafiti walioko vijijini waliiandaa jumuiya kwa ajili ya
utafiti wa uwandani na pia waliandaa majadiliano. Utafiti wa uwandani
huko Kamaziya katika Wilaya ya Binga ulitembelea kaya 40; huko
Plumtree takribani kaya 100 zilitembelewa. Matumizi
ya Rasilimali Katika
Wilaya ya Binga, wanaume hudhibiti rasilimali za familia na kuona
kwamba rasilimali hizo zinagawanywa na kutumiwa vema. Rasilimali hizi
hujumuisha ardhi, maji, mazao ya mimea, mifugo, na nguvukazi ya
familia. Ardhi hugawanywa kwa familia mpya na chifu wa eneo ambaye,
kwa kushauriana na wazee wengine, hugawanya ardhi kwa ajili ya makazi
na kilimo. Usimamizi wa ardhi na rasilimali zake katika Wilaya ya
Binga hufanywa na Kamati za Maendeleo za Vijiji zilizoanzishwa na
serikali miaka ya 1980. Wakazi
wa Wilaya ya Plumtree hujishughulisha zaidi na kilimo cha kujikimu na
ufugaji wa wanyama. Ingawa mbao ni nyingi, wakazi wa eneo hili huona
kuwa rasilimali hizi hazitumiwi kwa ufanisi kuwa chanzo cha ajira na
mapato. Mbao nyingi hutumika kama kuni na kwa ajili ya ujenzi wa
nyumba na nyua. Desturi
za Mifumo ya Maarifa ya Asili Mifumo
ya Maarifa ya Asili imo katika maeneo yote mawili na bado
inawahimilisha wanavijiji katika ukulima wa mazao - ikiwa ni pamoja na
utayarishaji wa ardhi, uchaguaji wa nafaka, upandaji, uvunaji, na
kadhalika uhifadhi wa nafaka na usimamizi wa mifugo. Desturi
iliyozoeleka zaidi ya mifumo ya maarifa ya asili ya Wakalanga ilihusu
maarifa yao ya asili ya nyasi na udongo unaofaa kutengwa kwa ajili ya
malisho. Viongozi wa familia walikutana nyumbani kwa chifu kila majira
ya kuchupua ili kujadili mipango ya malisho kwa majira hayo. Tarehe za
kuanza na kumaliza kuchungia katika malisho maalum pia zilipangwa
kisha wajumbe na wakuu wa vijiji walisimamia utekelezaji wa wanavijiji
wa kanuni hizi. Jumuiya
zote mbili za Binga na Plumtree walithamini mambo matatu kuhusiana na
mifumo ya maarifa ya asili. Kwanza, maarifa ni nguvu. Watu walioishi
Plumtree kwa miaka mingi walifahamu ruwaza za mvua na vipindi vya
kupanda mazao ili kupata mavuno mazuri. Thamani ya pili ya mifumo ya
maarifa ya asili ilihusu msingi wa maarifa unaowezesha ugawanyaji
mzuri wa chakula na pia mgawano mwafaka wa kazi. Jambo la tatu muhimu
mintarafu mifumo ya maarifa ya asili lilihusiana na upatikanaji wa
hudumu wa rasilimali kwa ajili ya maisha endelevu. Hitimisho Wakati
wa utafiti wake wa uwandani, mwandishi wa makala hii aligundua jinsi
jumuiya za wenyeji zinavyoithamini mifumo ya maarifa ya asili.
Makabila yote mawili ya Watonga na Wakalanga wanathamini mifumo ya
maarifa ya asili kama msingi wa maarifa na wa uzalishaji wa chakula na
ugawanaji wa kazi kati ya jinsia na marika na pia kama sehemu ya
uendelevu wa uhai wao. Mwandishi anapendekeza kwamba mifumo ya maarifa
ya asili ijalize, badala ya kushindana na ile ya Magharibi, katika
utekelezaji wa miradi. Funzo kwa mashirika ya kimaendeleo sharti liwe
kuchunguza kwanza nini wenyeji wanajua na wanacho, na kisha
kuziendeleza na kuziboresha teknolojia za asili. Katika
Wilaya ya Plumtree, wananchi walionyesha kwamba ukame unaotokea mara
kwa mara na kukosekana kwa nyasi na ardhi za malisho umefanya
uchungaji wa mzunguko, ambao ni wa mapokeo, kuwa ngumu. Athari za
Magharibi pia ziliitishia mifumo ya maarifa ya asili. Wilaya ya Binga
ilionyesha kuwa mbinu za kulima za asili zimeachwa na badala yake
zinatumika zile za Magharibi; mazao ya mapokeo yamebadilishwa na mazao
ya biashara. Moja
ya upungufu wa mifumo ya maarifa ya asili ni kukosekana kwa nyaraka
inayohusu mifumo hiyo. Maarifa ya Waafrika juu ya mimea ya asili
pamoja na majina yake yanapungua kwa kasi kubwa. Ubora wa mifumo ya
maarifa ya asili ni finyu pia kutokana na maarifa haya kutokitwa kwa
utafiti wa kisayansi. Kinachoelezwa zaidi ni kwamba ni mwiko kufanya
mambo fulani. Mifumo ya maarifa ya asili pia ina hatari ya kutoweka
kwa vile inategemea wale wanaohadhi maarifa hayo kuwa tayari kuwagawia
wenzao. Aidha vijana wengi huyaona maarifa haya kuwa yamepitwa na
wakati ikilinganishwa na maarifa ya utamaduni na desturi za Magharibi. Utafiti
unapendekeza mambo yafuatayo: ·
Andaa programu imara za utambuzi wa mifumo ya maarifa ya asili
na nafasi yake katika menejimenti (usimamizi) ya utumiaji wa
rasilimali. ·
Tafiti, weka katika nyaraka na sambaza taarifa za kina kuhusu
mifumo ya maarifa ya asili. ·
Kuza na hamishia mifumo ya maarifa ya asili kwenye maeneo yenye
sifa bainifu zinazofanana. Kutembeleana baina ya vikundi
vinavyoendesha miradi inayofanana ni njia mojawapo ya kutekeleza azima
hii, kama zifanyavyo warsha juu ya masuala muhimu ya mifumo ya maarifa
ya asili. ·
Toa machapisho juu ya mifumo ya maarifa ya asili, hasa katika
lugha za kienyeji za jumuiya lengwa. ·
Patia mafunzo wafanyakazi wa mashirika ya maendeleo, hasa wale
wanaofanya kazi moja kwa moja na jumuiya za asili. ·
Jenga uwezo wa wenyeji wa kutambua thamani ya mifumo ya maarifa
ya asili na kuza mifumo hii kupitia: mikusanyiko ya kimapokeo ya
jumuiya; mafunzo juu ya utafiti wa mifumo ya maarifa ya asili;
uandaaji nyaraka na usambazaji wake; na msaada toka sekta rasmi wa
kuziwezesha jumuiya za asili kuendeleza zenyewe mifumo ya maarifa ya
asili. Makala
hii iliandikwa na Harold Sibanda, Ofisa Mipango wa Umoja wa Vyama vya
Vijiji kwa Maendeleo ya Bulawayo, Zimbabwe. Imerudiwa kuchapishwa
kutoka Perspectives on
Indigenous Knowledge Systems in Southern Africa na Jeri Larson,
April 1998, Discussion Paper No.3, Environment Group, Africa Region,
WB. Kwa maelezo zaidi wasiliana na Jeri Larson, Rm J8 - 120, World
Bank, 1818 H Street, NW, Washington D.C 20433. Tel. No (202) 4734333. E-mail:
jlarson@worldbank.org |