THE WORLD BANK GROUP A World Free of Poverty
Home

[Back to TOC]

Senegal: Demokrasia ya Umma ikifanya kazi

Katika vijiji vya bonde la walima karanga wa Kiwolof na Wafulani wa Fouta Toro nchini Senegal , “demokrasia” limekuwa ni neno litumikalo na wengi. Shirika la Senegal lisilo la kiserikali (NGO) “Tostan” (jina la Kiwolof linalomaanisha kujitoa katika yai), ambayo ni programu ya elimu isiyo rasmi ya wanawake wa vijijini, kwa kipindi cha zaidi ya miaka miwili limekuwa likiendesha mafunzo ya misingi na mienendo ya demokrasia. Mpango huu umefuatia programu ya mafunzo na uwezeshaji ambayo imekuwa ikiendeshwa na NGO hii katika eneo lote la Senegal ya kati kwa muongo (miaka kumi) uliopita. Mpango huu ulikuwa wazi kwa watu wote, lakini uliwalenga hasa wanawake na ulijumuisha mafunzo katika utatuzi wa matatizo, uzalishaji mapato, kusoma na kuandika katika lugha ya Kiafrika na afya ya mtoto. Ili kukidhi mahitaji yaliyojitokeza na kadiri mpango ulivyokua, maudhui mapya ya mafunzo yalitayarishwa kwa kuwashirikisha wanafunzi walengwa. Mojawapo ya maudhui ya mwisho yalihusu afya ya wanawake, ikiwa ni pamoja na majadiliano juu ya somo nyeti lililoharamishwa – yaani nafasi ya wanawake katika ngono-mada iliyowavutia washiriki wengi vijijini kote. Wafanyakazi wa Tostan waligundua kwamba chanzo cha hamasa kubwa na yenye nguvu katika mada hii kilikuwa msisitizo wa mada juu ya haki za binadamu, hasa haki za wanawake na watoto kutobaguliwa na kutotishwa na vurugu. Watu walitaka kufahamu zaidi juu ya mambo haya.

Demokrasia kuanzia kwenye familia hadi kwenye ngazi ya Taifa  

Kabla ya kuandaa maudhui mapya, wafanyakazi wa NGO waliamua kufanya utafiti uliowashirikisha wananchi ili kujua mahitajio muhimu ya wananchi hao katika mafunzo ambayo yangetolewa. Matokeo ya utafiti yalikuwa ya kushangaza. Wananchi walihitaji sana kupanua uelewa wao wa masuala ya haki za binadamu na kuangalia kwa makini masharti yake na hata aina ya jamii, ambamo haki hizi zinaweza kutekelezeka kwa uthabiti zaidi. Neno “demokrasia” lilijitokeza mara nyingi, likiwa limesikika kutoka kwenye mjadala wa kisiasa wa kitaifa, lakini hakukuwa na mtu aliyekuwa na uhakika wa maana ya neno hilo. Hivyo wafanyakzi waliamua kufanya majaribio ya utaratibu wa mafunzo uliohusisha dhana ya demokrasia na mfumo wa kijamii uliopo ambamo haki za binadamu zinaweza kutekelezwa kwa ufanisi na watu wa aina zote wanaweza kushiriki kuamua majaliwa yao. Maudhui ya mafunzo yaliyotokana na majaribio haya yaliyodumu kwa miezi kadha yalijumuisha taarifa (habari), majadiliano, uigizaji na shughuli zenye matumizi yenye manufaa – vyote vikisisitiza juu ya haki za binadamu ambazo jamii lazima izilinde, jinsi maadili binafsi na ya vikundi yanavyowekwa sawa, kwa njia gani wale walionyang’anywa haki zao wanaweza kuzidai, jinsi gani mizozo hutatuliwa, na mikakati ya uongozi bora inayohitajika kwa ajili ya malengo ya aina hii. Waandaaji waliona ni vema kurejea maana ya msingi ya “demokrasia” katika Kigiriki – yaani serikali inayoendeshwa na watu – na kutoa nafasi kwa majadiliano mapana juu ya kilichomaanishwa hasa na dhana hii na jinsi ilivyohusishwa na madai ya haki za binadamu na utatuzi wa mizozo. Demokrasia ilifasiliwa na kujadiliwa kama mpango unaoathiri maisha ya familia na jumuiya za vijiji kama unavyoathiri pia siasa katika ngazi ya mkoa au taifa. Mjadala na mabadilishano ya mawazo juu ya mada hizi katika jumuiya zilizoshiriki ulikuwa wa kusisimua na punde ukavuka mipaka ya kozi ya elimu isiyo rasmi. Mazungumzo mengi ya pande mbili kati ya wanaume na wanawake, vijana na wazee, na hata baina ya kabila mbalimbali yalijitokeza katika maeneo mengi yaliyohusishwa kwenye mradi huu.

 Kutunza imani ya wananchi

Waandaaji walijali sana kushirikisha mamlaka za vijiji na viongozi wa kidini katika programu hii. Kusema kweli, pengine kichocheo kikuu cha mpango huu ulikuwa mwingiliano na maadili ya kidini, hasa ile ya Kiislamu, katika maeneo husika. Mtazamo wa waumini wengi ulikuwa kwamba haki na kanuni za kidemokrasia zilizokuwa zikijadiliwa ziliakisi vema zaidi maadili ya Kiislamu kuliko ya jamii ya kisasa au desturi za kileo.

 Matokeo ya dhahiri yalionekana punde katika nyanja mbalimbali. Msukumo mkubwa ulielekea kutokana na falsafa ya Gandhi ya kutotumia nguvu – yaani, kutokana na juhudi za makusudi za kuwafanya wananchi kutambua ukinzani kati ya maadili na mienendo halisi. Ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika familia unatoa mfano hai. Washiriki wa programu ya elimu ya demokrasia ya Tostan walishutumu tabia ya kuwapiga wake na watoto katika familia. Matukio halisi ya vipigo yalitolewa na kujadiliwa katika jumuiya mbalimbali. Kama kiongozi wa kiume wa kaya katika kijiji cha Ngaparou alivyosema “sote tulijua kwamba haikuwa haki kuwapiga wanawake. Tulifanya hivyo kwa mabavu tu. Lakini hatuna budi sasa kubadilika, kwa sababu jambo hili sasa linachukuliwa kuwa ni uovu na watu wote. Ni jambo lililo hadharani. “Kuwa hadharani” – ingawa kwa kawaida si kwa namna ya ushari – ndiyo imekuwa zana kuu ya mabadiliko haya”.

 Haki za watoto ni jambo jingine muhimu linalotiliwa mkazo. Vikundi vingi katika mji wa Thies vilivyoshiriki kwenye programu hii vilibaini kuwa kukosekana kwa vyeti vya kuzaliwa kwa watoto wengi katika jumuiya zao ilikuwa mojawapo ya ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu. Jambo hili lilipaswa kurekebishwa, kwani liliwazuia watoto hawa kujiandikisha shuleni na kupata fursa nyingine za maisha bora. Washiriki wa programu walishawishi uanzishwaji wa taratibu mpya na upatikanaji na vyeti vya kuzaliwa kwa idadi kubwa ya vijana. Katika baadhi ya maeneo ya mkoa, tatizo la ndoa za utotoni bila ridhaa ya wasichana lilijadiliwa pia kwa kina. Ongezeko la msisitizo juu ya haki za wasichana lilipelekea pia kwenye upigwaji marufuku tabia ya kutahiri wanawake – jambo lililojadiliwa kwenye IK Notes # 3 kuhusu Kiapo cha Malicounda.

 Desturi za uwajibikaji

Mjadala wa demokrasia unaelekea pia kuwa na athari kubwa kwa utendaji kazi wa vyama vya kijumuiya na jumuiya zenyewe. Dhana za uwajibikaji, uwazi, sifa za uongozi, uwakilishi wa vikundi mbalimbali na utawala bora zilijadiliwa sana kwenye mtaala kama ilivyokuwa pia kuhusiana na mbinu za kutatua mizozo inayoletwa na madai ya kutambulika kijamii na ya usawa. Wafanyakazi wa Tostan wanawaona washiriki wa awali wa programu hii wakikiri kuwa pamekuwepo na mabadiliko makubwa katika taratibu na hata watumishi wa vyama vya kijumuiya kutokana na mafunzo haya. “Sasa tunajua vizuri zaidi sifa za kiongozi”, wanasema: na kuna ongezeko kubwa la ushiriki wa wanawake katika shughuli za uongozi. Aidha wanawake hawataki tena kuvumilia utaratibu wa kijadi ambapo kiongozi – wa kiume au wa kike – hutoa maamuzi kwa ajili ya washirika wenzake. Na katika maeneo kadhaa vituo vya kutatua mizozo vimeanzishwa na wanawake waliohitimu mafunzo ya demokrasia.

Zaidi ya hayo, yapo pia madai mengine ya kisiasa. Washiriki wanadhani kuwa idadi kubwa zaidi ya wanawake wanapendelea kupiga kura kuliko ilivyokuwa hapo awali – na wachache wanaukubali utaratibu uliozoeleka ambapo kiongozi wa kiume wa kaya huwaelekeza wanafamilia wote jinsi ya kupiga kura. (Kwa hakika katika baadhi ya vijiji chifu ndiye aliyeamwua namna wakazi wake wote watakavyopiga kura). Mjadala juu ya sifa za kiongozi umepelekea kuanzishwa kwa vigezo vipya vya kuwatathimini wagombea wa nafasi za uongozi wa kisiasa katika baadhi ya maeneo. Orodha mahususi ya vigezo hivyo ilitayarishwa na wagombea wakahitajika kuwa na idadi kubwa ya vigezo hivyo kabla ya kuteuliwa kushika madaraka. Wanawake wa eneo la Fouta Toro waliazimia kufuatilia kwa karibu utungaji wa sheria za kitaifa ili uzingatie haki za binadamu.

Sekta inayokua

Dai la mafunzo ya demokrasia limekuwa likiongezeka na kuchochea ari ya kupigia kampeni masuala ya haki za wanawake. Washiriki kutoka visiwa vya Sine Saloum kiangazi hiki walitumia mitumbwi kuzifikia jumuiya mbalimbali katika eneo lao ili kuunda umoja dhidi ya tohara za wanawake. Zaidi ya vijiji themanini, vilivyoenea takribani katika tarafa nzima ya Dabo, vimejiunga na umoja huu kwa hiari yao. Na katika maeneo ya Toucouleur ya Fouta Toro washiriki wa programu ya mafunzo wameanzisha “maonyesho ya barabarani” ambayo huonyeshwa kwenye vijiji mbalimbali vya maeneo hayo.

Matokeo yameonekana pia kwenye maeneo ya mbali kabisa. Washiriki kutoka eneo la Ngirin Bamba walianzisha mradi wa bustani kwa kuomba mashamba kutoka kwa wanaume wa kijijini kwa msingi wa “ardhi kwa mkulima” – na kisha wakaweka bango kwenye lango la bustani yao ya mboga za majani na matunda lililosomeka “haki ya kumiliki ardhi”.

Hivyo dhana za “demokrasia” – zinazozingatia mazingira halisi ya Senegal zinajumuishwa katika madai haya mbalimbali ya haki za binadamu. Neno lenyewe limekopwa moja kwa moja katika lugha za Kiwolof na Kifulani/Kipulaar na kutumika mara kwa mara katika mabishano, matangazo, na utani kwenye vijiji vyote vinavyoshiriki katika programu ya mafunzo. Kama mwanamke mmoja wa Ker Simbara alivyomweleza mwendesha mafunzo aliyetembelea huko kufuatilia utekelezaji wa programu, “tulilazimika kubadilisha uendeshaji wa mikutano yetu ya ushirika kwa sababu tulibaini kuwa ilikuwa haiendani na “demokrasia”. Wakati majaliwa ya serikali ya uwakilishi wa kitaifa yangali mashakani katika bara lote la Afrika, iaelekea demmokrasia inayozingatia mazingira halisi ya eneo husika ndiyo itakayopendelewa na nchi nyingi siku za usoni.

*Msingi wa makala hii ni utafiti uliofanywa na watafiti wa Senegal kwa msaada na ushauri wa kiufundi wa Profesa Peter Eastom wa Chuo Kikuu cha Jimbo la Florida, wakishirikiana na baadhi ya jumuiya za Kiafrika. Utafiti ulifadhiliwa na Club du Sahel OECD, CILSS na ADEA.

[Back to TOC]


Footer