Matumizi
ya Elimu ya Kurani katika Nchi za Afrika Magharibi
Ni
stadi zipi halisi ambazo wanafunzi huzipata katika viwango mbalimbali
vya elimu ya kurani huko Afrika Magharibi? Kuna matumizi gani ya kila
siku ya elimu hiyo na mitandao gani hutumika katika kuikuza na kuitumia
elimu hiyo? Elimu ya kurani katika aina zake mbalimbali kwa muda mrefu
umekuwa mfumo sambamba wa elimu katika bara lote la Afrika – mfumo ambao
umekuwepo kwa karne nyingi, lakini bado haufahamiki sana na wataalam
wa mipango ya maendeleo na hivyo kwa nadra sana huzingatiwa katika sera
na mikakati ya wataalam hao.
Uislamu
una historia ndefu Afrika Magharibi na mifumo ya elimu ya kiislamu kwa
hakika imekuwa ikitumika huko kwa muda mrefu zaidi kuliko ile ya Magharibi.
Imani ya Kiislamu iliingia kwa mara ya kwanza huko Afrika ya Kaskazini
kwenye karne ya 7. Ilipofikia karne ya 10, jumuiya za wafanyabiashara
na wasomi wa Kiislamu zilikuwa tayari zinaishi kwenye vituo vya kibiashara
vya Sahara ya Magharibi na Sahel. Ilipofikia karne ya 11 au ya 12, watawala
wa falme kama vile za Takrur, Ghana ya Kale na Gao, tayari walikuwa
wameshasilimu na kuwateua Waislamu wajuzi wa Kiarabu kuwa washauri wao.
Biashara
ya kuvuka Jangwa la Sahara ilishamiri zama za kabla ya ukoloni na ikahusisha
idadi kubwa zaidi ya bidhaa zilizobadilishwa kati ya Afrika na Ulaya
kuanzia karne ya 11 hadi ya 16 – yaani hadi kabla ya kuwasili vyombo
vya Ulaya kwenye Pwani ya Afrika Magharibi na kuanzishwa kwa biashara
ya utumwa ya kuvuka Bahari ya Atlantiki na biashara ya pembe mraba baina
ya Afrika, Ulaya na Dunia Mpya iliyokuwa matokeo ya biashara ya kuvuka
Sahara. Awali msingi wa biashara ya kuvuka Sahara ulikuwa mitandao ya
miji iliyoanzishwa kwenye njia za biashara na wafanyabiashara kutoka
Afrika Kaskazini, ambao hatimaye walilowea na/au nafasi yao ikachukuliwa
na wenyeji. Kodi iliyotokana na biashara hii ilichangia sana kwenye
mapato yaliyohitajika kwa ajili ya ujenzi wa nchi/dola.
Muundo
wa Mfumo wa Mafunzo ya Kurani
Mfumo
wa mafunzo ya Kiislamu katika Afrika Magharibi nzima unajumuisha ngazi
kadhaa ingawa haziko waziwazi mno kama zile za mfumo wa Ulaya Magharibi.
Zaidi ya hapo, kwa sasa unajumuisha
muundo wa kimapokeo (mfululizo asilia wa mafunzo ya Kurani), shule rasmi
au ya “kisasa” (shule za mchanganyiko wa Kifaransa na Kiarabu, pengine
huitwa ‘madrasa’), na vidato vya kati ambavyo hujulikana kama “elimu
ya kurani iliyoboreshwa”. Ngazi ya chini kabisa ya muundo wa kimapokeo
ni ‘maktab’ au shule za Kurani za ngazi ya msingi ambako watoto wa miaka
3 hadi 10 huanza kujifunza Kurani na majukumu ya msingi ya maisha ya
Kiislamu. Ngazi inayofuata ni ya ‘madris’ au shule za sekondari ambako
wale waliomudu kukariri na kunukuu sehemu kubwa ya Kurani huendelea
kusoma kile kinachojulikana kama “sayansi ya Kiislamu” (‘ilm’), ikiwa
ni pamoja na maandiko muhimu ya dini na taaluma nyinginezo. Wanafunzi
wachache huendelea mbele kwa mafunzo ya juu zaidi chini ya maimamu na
mamurabiti mashuhuri au katika vyuo vikuu vya Kiislamu vya Afrika Kaskazini
na nchi nyingine za Kiislamu.
Walau
katika ngazi ya msingi – inayowakilishwa na shule za kurani za maeneoni
– mafunzo ya Kiislamu yameenea kote Afrika Magharibi. Huko Niger peke
yake kulikadiriwa kuwepo na takribani shule 40,000 za kurani mwaka 1990.
Aina hii ya elimu ni maarifa muhimu mbadala (wa elimu rasmi na ya Magharibi)
na aghalabu huchanganyika na pengine kushindana na elimu rasmi, ingawa
katika nchi nyingi za Afrika asasi za msingi za mfumo wa Kiislamu yaani
‘maktab’ – hazijachukuliwa kama shule kabisa. Pamoja na hayo, wanafunzi,
walimu na waumini wa Kurani kote Afrika Magharibi wanatambua fika historia
ndefu ya imani yao na wasomi na walimu wake mashuhuri, baadhi yao wakiwa
na madaraka makubwa ya kisiasa na kiuchumi, hasa katika eneo la Sahel.
Mathalani, wale wanaojishughulisha kwa miaka mingi na biashara ya mazao
huko Niger, Mali na Senegal wameimarisha mitandao ya biashara ya mitaji
mikubwa hasa katika sekta ya mashamba na viwanda nchini mwao, na pia
nchi za nje. Mambo yote haya yanazidi kuwa kivutio kwa elimu mbalimbali
za Kurani kama mfumo mbadala wa kufikia usitawi wa kiuchumi au kisiasa.
Kwa ufupi, kuna mwingiliano mkubwa wa utamaduni baina ya mataifa.
Ubora
unaotofautiana, uenea mkubwa
Licha
ya hali hii ya kufanana kimsingi kwa utamaduni na mafunzo ya kidini,
hali halisi na ubora wa mafunzo katika shule za Kurani na mfumo wa Kiislamu
kwa ujumla hutofautiana sana kutoka sehemu moja hadi nyingine. Katika
sehemu zenye waumini wengi wa Kiislamu, idadi kubwa zaidi ya watoto
huhudhuria shule za Kurani. Kimsingi hawa hujifunza kupitia mbinu ya
kukariri msahafu. Wengi wa wanafunzi ni wavulana, lakini aghalabu kwa
uwiano usiozidi 3/2 au 2/1 katika ngazi za mwanzoni. Katika sehemu chache
kama vile Futa Jalon huko Guinea, idadi ya wavulana na wasichana kwa
jumla ni kama imelingana.
“Kina”
cha mafunzo ya Kiislamu katika maeneo haya ni tofauti sana, lakini kwa
kawaida idadi ya kutosha ya wanafunzi wavulana wanaendelea baada ya
masomo ya awali ya Kurani hufikia hadi ngazi fulani za elimu ya juu.
Kwa kuwa uelewa wa Kiarabu cha kisasa ama cha kimapokeo nje ya msahafu
wenyewe ni mdogo sana, (isipokuwa kwa wale waliosomea kwenye nchi zinazozungumza
Kiarabu), kiwango cha juu kabisa cha uelewa – yaani, uwezo wa kusoma
na kuandika, kuweka rekodi na maandiko mbalimbali kwa ujumla – hupatikana
aghalabu kwenye nyanda za juu za Guinea, eneo la Sine Saloum la Senegal,
na maeneo ya wazungumzaji Kihausa ya Niger, ambako kuna mfumo wa unukuzi
ulioendelea wa lugha za Kiafrika unaotumia herufi za Kiarabu (ambazo
huitwa ‘ajami’ katika Kihausa na Kifulani). Nchini Guinea, asilimia
93 kati ya wahitimu wanaume 77 wa Kurani waliohojiwa walidai kuweza
kusoma na kuandika katika ‘ajami’. Nchini Senegal, kati ya asilimia
25 na 75 ya wanaume waliohojiwa vijijini, na kati ya asilimia 10 na
25 ya wanawake, walidai kuwa na kiwango sawa cha uelewa. Kwa kila hali,
kiwango hiki cha uelewa kwa jinsia zote mbili kilizidi uelewa wa Kifaransa
kwa jumuiya hizi ambazo kimsingi ni za vijijini.
Kwa
upande mwingine, asilimia 26 tu ya sampuli ya Guinea ya wanafunzi wa
zamani wa Kurani walijichukulia wanajua “kuhesabu” ikilinganishwa na
asilimia 93 waliojichukulia kuwa wanaweza kuandika katika ‘ajami’. Hata
hivyo, wengi wa mamurabiti na maimamu yaelekea walijifunza kuhesabu
kwa namna moja au nyingine, jambo linaloelezea sababu za kuwakuta wengi
wao wakishughulikia masuala ya mahesabu ya fedha katika jumuiya nyingi.
Wakati
ufundi stadi hauzingatiwi sana katika mafunzo ya Kurani, wengi wa wanafunzi
wanaoendelea na masomo baada ya yale ya msingi hujikuta wakifanya uanagenzi
chini ya mamurabiti ama mafundistadi au wafanyabiashara, ili kupata
fedha za kujikimu na kugharamia masomo. Elimu ya Kurani huelekea kuwa
na kipengee cha mafunzo ya mazoezi katika jumuiya, ingawa huchukua sura
ya mafunzo ya kiufundi stadi wakati mwingine; na wanafunzi wa Kurani
hujazwa na dhana kwamba watahitajika kujitegemea wenyewe au kutafuta
wafadhili mwafaka watakapofikia umri fulani. Hii ndiyo iliyompelekea
mtafiti mmoja wa Kisenegal kusema “shule za Kurani hufundisha wabunifu
wa ajira, ilihali mfumo wa elimu rasmi hufundisha watafutaji wa ajira”.
Matumizi
ya Mafunzo ya Kurani
Matumizi
makuu binafsi ya mafunzo ya Kurani ni kuandika na kuwasiliana, na ajira
maarufu kabisa kwa wahitimu waliobobea wa Kurani ni kuwa mamurabiti
au maimamu , kwa vile kuna mahitaji makubwa ya walimu na wahudumu wa
kidini; kutokana na kuenea kwa haraka kwa Uislamu huko Afrika Magharibi
kwenye miaka ya hivi karibuni. Hata hivyo zaidi ya robo ya wahojiwa
wa Guinea walisema kuwa ajira katika sekta ya huduma za umma ni matokeo
ya mafunzo yao. Dai hili hujitokeza pia katika eneo zima la Afrika Magharibi.
Hata
hivyo, yapo pia matumizi ya pamoja kwa kiwango cha kutosha. Maadili,
sheria na mamlaka ya Kiislamu yametumika sana kama msingi wa uongozi
wa kimapokeo kwa karne nyingi katika eneo lote la Sahel. Kusema kweli,
msamiati mwingi katika lugha kuu za Kisahel sio tu unahusu dini, bali
pia sheria, utawala, itifaki na elimu ya juu na hali kadhalika umetokana
moja kwa moja na Kiarabu ama umekopa manenno mengi toka lugha hiyo.
Hitimisho:Njia
mbadala za kupatia elimu
Kutokana
na hali iliyoelezwa hapo juu, mafunzo ya msingi ya Kiislamu – yale yanayotolewa
katika shule za Kurani – yana matumizi na athari za aina tatu kuu katika
Afrika Magharibi hivi leo:
·
Hutoa msingi
wa teknolojia ya kuandika – na kwa kiasi fulani, ya kuhesabu – kwa idadi
ya kutosha ya wananchi, wanaume na wanawake, ambao, vinginevyo wengi
wao wangekuwa na elimu ndogo kabisa ama wasingekuwa na elimu.. Wale
wanaojiendeleza na kuwa mahiri katika kusoma, kuandika na kuhesabu (hasa
katika lugha za Kiafrika, kwa vile umahiri katika Kiarabu ni ngumu zaidi)
kwa kawaida huwa ni wachache, ingawa katika baadhi ya maeneo idadi yao
ni kubwa kidogo. Zaidi ya hapo, kufahamu maandiko ya Kiarabu sasa hivi
huchukuliwa na watu wengi vijijini na mijini kuwa ni hali ya “kutoelimika”
kwa mtazamo wa kimagharibi.
·
Huchukuliwa
pia kuwa ni mafunzo kwa ajili ya uongozi, kwa vile mafunzo halisi ya
Kiislamu kwa kawaida huchukuliwa kuwa ni kionyeshi cha uadilifu, uaminifu
na nidhamu na hivyo kuwa sifa muhimu ya mtu kupatiwa nafasi ya madaraka.
·
Zaidi ya hapo,
mafunzo hayo daima yamekuwa – na kutokana na chuki ya hivi karibuni
dhidi yya elimu rasmi, yamezidi kuwa – daraja la kupatia maendeleo ya
kijamii na kiuchumi kutokana na uhusiano wa karibu kati ya mitandao
ya Kiislamu na ile ya biashara ya kimapokeo katika eneo lote. Wahitimu
wa shule za Kurani wana nafasi kubwa zaidi ya kupata ajira au uanagenzi
kutoka kwa wafanyabiashara wa kimapokeo na katika sekta isiyo rasmi
ya uchumi.
*Msingi
wa makala hii ni utafiti uliofanywa na watafiti wa Senegal kwa msaada
na ushauri wa kiufundi wa Profesa Peter Easton wa Chuo Kikuu cha Jimbo
la Florida, wakishirikiana na baadhi ya jumuiya za Kiafrika. Utafiti
ulifadhiliwa na Club du Sahel?OECD, CILSS na ADEA.